• HABARI MPYA

    Thursday, April 06, 2023

    NAIBU WAZIRI WA MICHEZO, MWANA FA AKUTANA NA KATIBU MKUU WA CAF


    MAIBU Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamisi Mohamed Mwinjuma ‘Mwana FA’ amekutana na kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF), Veron Mosengo-Omba.
    Katika mkutano huo ulifanyika leo Aprili 6, 2023 Durban nchini Afrika Kusini, Mhe. Mwinjuma ametumia fursa hiyo kwa niaba ya Serikali
    kuiomba CAF iangalie namna itakavyoiwezesha Tanzania ikishirikiana na Kenya na Uganda kuandaa mashindano ya AFCON mwaka 2027 kwa pamoja.
    Amesema hatua hiyo inatokana na mashindano hayo kutowahi kufanyika katika ukanda wa Afrika Mashariki. 
    Aidha Mhe. Mwinjuma amewasilisha ombi la Serikali la kuwa mwenyeji katika upangaji wa timu (Draw) ya mashindano ya Super Cup pamoja na kuwa mwenyeji wa mchezo wa kwanza wa mashindano hayo yanayotarajiwa kuanza mwezi Novemba, 2023 na kama ikitokea nafasi ya kuongeza timu basi CAF iipatie kipaumbele timu ya Yanga.
    Katika mazungumzo hayo  Mhe. Mwinjuma pia amefikisha salaam za shukrani za Serikali ya Tanzania kwa CAF kukubali kuufanyia marekebisho Uwanja Benjamin Mkapa baada ya timu ya Simba kuchaguliwa kushiriki mashindano ya Super League.
    Kwa Upande wake Katibu Mkuu wa (CAF), Veron Mosengo-Omba ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano inaoutoa kwa maendeleo ya mpira wa miguu Barani Afrika akamhakikishia Naibu Waziri, Mwinjuma kwamba CAF itaendelea kushirikiana na Tanzania.
    Aidha ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuwa na utayari wa kuandaa mashindano ya AFCON ya Mwaka 2027 kwa pamoja na nchi za Uganda na Kenya.
    Aidha, ametoa wito kwa nchi za Afrika Mashariki  ziwasilishe maombi mapema kwa kuwa mashindano ya SUPER CUP hayajawahi kufanyika katika ukanda wa Afrika Mashariki akibainisha kuwa maombi yameanza kupokelewa kuanzia Aprili 5, 2023 na yanatarajiwa  kufungwa baada ya siku 21.
    Kuhusu kuiongeza timu ya Yanga katika mashindano ya Super League Katibu wa CAF amemueleza Mhe. Mwinjuma kuwa kwa sasa wamechukua timu chache lakini baadaye Tanzania itaingiza timu mbili ambazo ni Simba na Yanga.


    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NAIBU WAZIRI WA MICHEZO, MWANA FA AKUTANA NA KATIBU MKUU WA CAF Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top