• HABARI MPYA

    Friday, October 01, 2021

    KAGERE AING'ARISHA SIMBA DODOMA


    BAO la mshambuliaji Mnyarwanda mwenye asili ya Uganda, Meddie Kagere dakika ya 70 limewapa ushindi wa kwanza mabingwa watetezi, Simba SC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara dhidi ya wenyeji, Dodoma Jiji FC jioni ya leo Uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.
    Kagere amefunga bao hilo dakika saba tu tangu aingie kuchukua nafasi ya mchezaji mpya, Yussuf Mhilu akimalizia pasi ya kichwa mshambuliaji Mkongo, Chris Kope Mutshimba Mugalu kwa guu lake la kulia kufuatia mpira mrefu ulioanzishwa na kipa Aishi Salum Manula.
    Simba inafikisha pointi nne baada ya mechi mbili za mwanzo kufuatia sare ya bila mabao na wenyeji, Dodoma Jiji FC kwenye mechi ya kwanza Jumanne mjini Musoma mkoani Mara.
    Dodoma Jiji FC inayofundishwa na kipa wa Yanga miaka ya 1980, ilimaliza pungufu kufuatia mshambuliaji wake, Anuary Majjid Jabir kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 41 baada ya kumpika kiwiko beki wa Simba, Kennedy Wilson Juma.
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, bao la winga wa zamani wa Simba SC, Rashid Juma dakika ya 47 limeipa Ruvu Shooting ushindi wa 1-0 pia dhidi ya wenyeji, Biashara United Uwanja wa Karume mjini Musoma.
    Ni ushindi wa kwanza wa Ruvu baada ya kuchapwa 1-0 na Dodoma Jiji kwenye mechi ya kwanza, wakati hali si shwari kwa wawakilishi wa Tanzania kwenye Kombe la Shirikisho Afrika wakiambulia pointi moja kwenye mechi mbili za awali nyumbani.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KAGERE AING'ARISHA SIMBA DODOMA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top