• HABARI MPYA

    Wednesday, November 18, 2020

    TAIFA STARS YALAZIMISHWA SARE YA KUFUNGANA BAO 1-1 NA TUNISIA KUFUZU AFCON YA MWAKANI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM 
    TANZANIA imezidi kujiweka kwenye nafasi ngumu ya kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) baada ya kulazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na Tunisia katika mchezo wa Kundi J usiku huu Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Kwa matokeo hayo, Tunisia wanafikisha pointi 10 na kuendelea kuongoza kundi hilo, sasa wakiwazidi pointi nne Equatorial Guinea wanaofuatia, wakati Tanzania inafikisha pointi nne na kusogea nafasi ya tatu ikiiteremshia mkiani Libya yenye pointi tatu baada ya timu zote kucheza mechi nne.
    Hadi mapumziko, Carthage Eagles walikuwa mbele kwa 1-0, bao lililofungwa na kiungo wa Olympique de Marseille ya Ufaransa, Saif-Eddine Khaoui dakika ya 11 akitumia makosa ya safu ya ulinzi ya Taifa Stars.



    Na dakika mbili baada ya kuanza kipindi cha pili Taifa Stars ikasawazisha kupitia kwa kiungo wa Yanga SC, Feisal Salum Abdallah ‘Fei Toto’ kwa shuti la umbali wa mita 20 kufuatia pasi ya kifua ya mshambuliaji na Nahodha, John Bocco/Adam Omary dk53 baada ya krosi ya Ditram Nchimbi kutoka kulia.
    Tunisia waliendelea kutawala mchezo na kucheza kwa utulivu pamoja na kuwaruhusu Taifa Stars kupata bao ka kusawazisha, lakini sifa zimuendee kipa Aishi Manula aliyeokoa michomo kadhaa.
    Taifa Stars nayo ilitengeneza nafasi nzuri zaidi ya tatu za kufunga mabao lakini wakapoteza kupitia kwa Iddi Suleiman ‘Nado’, Adam Omary na Ditram Nchimbi. 
    Kikosi cha Tanzania kilikuwa; Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Erasto Nyoni, Bakari Mwamnyeto, Jonas Mkude, Himid Mao/Feisal Salum dk35, Ditram Nchimbi, John Bocco, Simon Msuva/Said Ndemla dk80 na Farid Mussa/Iddi Suleiman ‘Nado’ dk80.
    Tunisia; Farouk Ben Mustapha, Wajdi Kechrida/Mohamed Drager dk79, Yassine Meriah, Dylan Bronn, Youssef Msakni/ Nabil Makni dk90, Saif-Eddine Khaoui/Naim Sliti dk69, Wahbi Khazri/Hamza Rafia dk77, Ali Maaloul, Ferjani Sassi, Mohamed Ben Amor/Anis Ben Slimane dk90 na Ellyes Skhiri.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TAIFA STARS YALAZIMISHWA SARE YA KUFUNGANA BAO 1-1 NA TUNISIA KUFUZU AFCON YA MWAKANI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top