• HABARI MPYA

    Tuesday, January 07, 2020

    YANGA SC YATINGA NUSU FAINALI KOMBE LA MAPINDUZI BAADA YA KUICHAPA JAMHURI 2-0, ITAMENYANA NA MTIBWA SUGAR

    Na Mwandishi Wetu, ZANZIBAR
    YANGA SC imefanikiwa kutinga Nusu Fainali ya michuano ya Kombe la Mapinduzi baada ya ushindi wa 2-0 dhidi ya Jamhuri ya Pemba usiku huu Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Ushindi wa Yanga SC wa leo umetokana na mabao ya nyota wake Kizanzibari, beki Adeyoum Saleh Ahmed dakika ya 45 na ushei na kiungo Mohammed Issa Juma ‘Banka’ dakika ya 85.
    Sasa Yanga SC itamenyana na Mtibwa Sugar ya Morogoro Alhamisi Saa 2:15 usiku katika Nusu Fainali Uwanja wa Amaan. Mtibwa yenyewe jana iliitoa Chipukizi ya Pemba kwa penalti 4-2 baada ya sare ya 1-1 jana Uwanja wa Gombani.


    Nusu Fainali nyingine itaikutanisha Simba SC na Azam FC Ijumaa Uwanja wa Amaan, Zanzibar kuanzia Saa 2:15 usiku. Hiyo ni baada ya mabingwa hao wa Tanzania kuwatupa nje Zimamoto ya Zanzibar kwa kuwachapa mabao 3-1 jioni ya leo Uwanja wa Gombani, Pemba.
    Mabao ya Simba SC leo yamefungwa na Nahodha wake, mshambuliaji John Raphael Bocco dakika ya tano na viungo, Msudan Sharaf Eldin Shiboub dakika ya tisa na mzawa, Ibrahim Ajibu dakika ya 54, wakati bao pekee la Zimamoto limefungwa na Ibrahim Ahmad ‘Hilika’ dakika ya 29.
    Azam FC yenyewe ilitangulia Nusu Fainali jana baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya Mlandege SC, bao pekee la mshambuliaji wake Mzambia, Obrey Chirwa dakika ya 57 Uwanja wa Amaan.
    Nusu Fainali hiyo itakuwa sawa na marudio ya fainali ya michuano hiyo mwaka jana Uwanja wa Gombani, ambayo Azam FC iliibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya Simba SC wakati huo ikiwa chini ya kocha Mbelgiji Patrick Aussems.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YATINGA NUSU FAINALI KOMBE LA MAPINDUZI BAADA YA KUICHAPA JAMHURI 2-0, ITAMENYANA NA MTIBWA SUGAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top