• HABARI MPYA

    Wednesday, January 22, 2020

    YANGA SC YAZINDUKA LIGI KUU BAADA YA KUICHAPA SINGIDA UNITED 3-1 LEO UWANJA WA LITI

    Na Mwandishi Wetu, SINGIDA
    KLABU ya Yanga imezinduka baada ya ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya wenyeji, Singida United katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Liti, zamani Namfua mkoani Singida.
    Ushindi huo wa kwanza ndani ya mechi nne, wakitoka kufungwa mechi mbili na sare moja, unaiongezea Yanga pointi tatu na kufikisha 28 katika mchezo wa 15, hivyo kupanda hadi nafasi ya nne.
    Kwa sasa inalingana kwa pointi na Namungo FC, iliyocheza mechi 15 pia, wote wakiwa nyuma ya Coastal Union yenye pointi 30 za mechi 17, Azam FC pointi 35 za mechi 16 na mabingwa watetezi, Simba SC wenye pointi 41 za mechi 16.


    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Omary Mdose aliyesaidiwa na Mohamed Mkono, wote wa Tanga na Leonard Mrumbo wa Manyara, hadi mapumziko, Yanga SC inayofundshwa na kocha Mbelgiji Luc Eymael ilkuwa mbele kwa mabao 1-0.
    Aliyefungua shangwe za mabao leo alikuwa ni mshambuliaji kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), David Molinga Ndama ‘Falcao’ dakika ya 11 akimalizia pasi ya kiungo Mapinduzi Balama baada ya krosi ya winga Mghaha, David Morrison.    
    Kipindi cha pili kiungo mkongwe wa kimataifa wa Rwanda, Haruna Hakizimana Fadhil Niyonzima alifumua shuti kumtungua kipa Mmalawi, Owen Chiama dakika ya 55 akimalizia krosi ya Morrison.
    Na kwa mara nyingine, Morrison akatia mpira wa juu langoni mwa Singida United uliomaliziwa kwa kichwa na mshambuliaji Yikpe Gilsaina Gnamien kuipatia Yanga bao la tatu dakika ya 80.
    Mshambuliaji mpya, Sixtus Mwasekaga akaifungia bao la kufutia machozi Singida United kwa kichwa dakika ya 85 akimalizia krosi ya kiungo wa zamani wa Yanga, Athumani Iddi ‘Chuji’.
    Kikosi cha Singida United kilikuwa; Owen Chiama, Aaron Lulambo/Athumani Iddi ‘Chuji’ dk86, Mwinyi Mngwali, Tumba Swedi, Daudi Mbweni, Kazungu Mashauri/Stephen Opoku dk30, Elinywesia Sumbi, George Sangija/Emmanuel Maziku dk50, Six Mwasekaga, Haruna Moshi na Erck Mambo.
    Yanga SC; Metacha Mnata, Juma Abdul, Jaffar Mohamed, Lamine Moro, Said Juma ‘Makapu’, Papy Kabamba Tshishimbi, Deus Kaseke/Abdul Aziz dk78, Haruna Niyonzima, David Molinga/Yikpe dk66, Bernard Morrison/Erick kabamba dk90+ na Mapinduzi Balama. 
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, Azam FC ya Dar es Salaam imeibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Mwadui FC Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga, bao pekee la mshambuliaji wake, Shaaban Iddi Chilunda dakika ya 20 katika mchezo ambao wenyeji walipoteza mkwaju wa penalti baada ya Gerald Mathias kupiga nje dakika ya tano.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YAZINDUKA LIGI KUU BAADA YA KUICHAPA SINGIDA UNITED 3-1 LEO UWANJA WA LITI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top