• HABARI MPYA

    Saturday, January 18, 2020

    SONSO AJIFUNGA, ATOLEWA KWA KADI NYEKUNDU YANGA SC YACHAPWA 1-0 NA AZAM FC TAIFA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Azam FC imefanikiwa kuibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya vigogo, Yanga SC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara usiku huu Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.
    Shukrani kwa beki mpya, Ally Abdulkarim Mtoni ‘Sonso’ aliyejifunga kipindi cha kwanza na kwa ushindi huo, Azam FC inayomilikiwa na Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa na familia yake inafikisha pointi 32 katika mchezo wa 15 na kurejea nafasi ya pili, ikizidiwa pointi sita na mabingwa watetezi, Simba SC.
    Chonso alijifunga dakika ya 25 kuipatia Azam FC bao hilo pekee baada ya kugongwa kwenye magoti na mpira uliopanguliwa na kipa Mkenya Farouk Shikaro kufuatia kona ya beki Mzimbabwe, Bruce Kangwa na kutinga nyavuni.


    Lakini Yanga hawakukata tamaa baada ya bao hilo na waliendelea kucheza vizuri, wakipeleka mashambulizi mfululizo langoni mwa Azam FC, lakini wakakosa mipango mizuri ya umaliziaji, kutokana na wapinzani wao kuwa wengi kwenye eneo lao muda mwingi.
    Kipindi cha pili, mambo yakazidi kuiharibikia Yanga baada ya beki wake, Ally Mtoni kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya kwa kumchezea rafu beki Mganda wa Azam FC, Nico Wadada.
    Na kiungo Papy Kabamba Tshishimbi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ambaye pia ni Nahodha, akashindwa kumalizia dakika za nyongeza baada ya kuumia dakika ya 90 na kutoka uwanjani anachechemea, nafasi yake ikichukuliwa na Said Juma ‘Makapu’.
    Huo ni mchezo wa pili mfululizo Yanga inapoteza nyumbani, baada ya Jumatano kuchapwa 3-0 na Kagera Sugar na kwa ujumla ni mwanzo mbaya mno kwa makocha wapya, Mbelgiji  Mbelgiji Luc Eymael na Msaidizi wake, Riedoh Berdien raia wa Afrika Kusini baada ya kupoteza mechi zote mbili za mwanzo kazini.
    Kikosi cha Azam FC kilikuwa; Razack Abalora, Nico Wadada, Bruce Kangwa, Daniel Amoah, Oscar Maasai, Joseph Mahundi, Bryson Raphael, Salum Abubakar ‘Sure Boy’, Iddi Suleiman ‘Nado’/ Masoud Abdallah ‘Cabaye’ dk90+3, Shaban Iddi Chilunda/ Donald Ngoma dk78 na Obrey Chirwa/ Never Tigere dk67.
    Yanga SC; Farouk Shikaro, Juma Abdul, Jaffar Mohamed, Lamine Moro, Ally Mtoni ‘Chonso’, Papy Kabamba Tshihimbi/ Said Juma ‘Makapu’ dk89, Deus Kaseke, Haruna Niyonzima, David Molinga, Patrick Sibomana/Ditram Nchimbi dk57 na Mapinduzi Balama/ Yikpe Gislain dk76.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SONSO AJIFUNGA, ATOLEWA KWA KADI NYEKUNDU YANGA SC YACHAPWA 1-0 NA AZAM FC TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top