• HABARI MPYA

    Friday, September 29, 2017

    YANGA NA MTIBWA SUGAR SHUGHULI PEVU UHURU KESHO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL), inatarajiwa kuendelea kesho kwa Yanga SC kuikaribisha Mtibwa Sugar Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.
    Yanga ambayo tayari imekusanya pointi nane inachuana na kinara huyo wa Ligi Kuu ya Vodacom tangu ianze, Mtibwa Sugar ya Morogoro ambayo hadi sasa imekusanya pointi 10. Timu zote zimecheza mechi nne hadi sasa.
    Mbali ya mchezo huo utakaochezwa Uwanja wa Uhuru Dar es Salaam, mechi nyingine za kesho zitakuwa ni kati ya Ndanda itakayokuwa mwenyeji wa Lipuli FC kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara. Ndanda ina pointi nne ilihali Lipuli ina pointi tano.
    Maji Maji ambayo ina pointi mbili baada ya mechi nne, inaikaribisha Kagera Sugar inayoshika mkia katika msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom kwa kupata pointi moja baada ya mechi nne. Mchezo utafanyika Uwanja wa Majimaji mjini Songea.
    Azam FC ambayo inafungana pointi na Mtibwa Sugar kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kesho itakuwa mgeni wa Singida United kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma. Singida United ina pointi tisa baada ya mechi nne.
    Mbeya City imesafiri moja kwa moja hadi Shinyanga ambako kesho inacheza na Mwadui kwenye Uwanja wa  Mwadui. Mbeya City imekusanya pointi sita hadi sasa baada ya mechi nne ilihali wenyeji wao Mwadui hadi sasa wana pointi tatu.
    Ndani ya Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza, Mbao FC itaikaribisha Tanzania Prisons ya Mbeya kwenye mchezo mwingine wa VPL. Rekodi zinaonesha kwamba Mbao FC hadi sasa ina pointi nne wakati Tanzania Prisons ina pointi nane.
    Uwanja wa Mabatini uliko Mlandizi mkoani Pwani, Ruvu Shooting FC itachuana na Njombe Mji katika mchezo mwingine wa VPL. Ikumbukwe tu kwamba hadi sasa baada ya mechi nne, timu hizo - Ruvu Shooting na Njombe Mji zote zimekusanya pointi tatu.
    Kama ilivyodokezwa kwenye aya ya pili hapo juu, keshokutwa Jumapili kutakuwa na mchezo mmoja tu wa VPL ambako Simba itakuwa mgeni wa Stand United ya Shinyanga katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga.
    Baada ya Ashanti United na Friends Rangers kugawana pointi kufuatia sare ya 2-2 leo, Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara itaendelea kesho Jumamosi kwa JKT Ruvu na Kiluvya United kumenyana Uwanja wa Mbweni katika mchezo mwingine wa kundi A.
    Kundi B kutakuwa na michezo miwili ambako Mufindi United itacheza na Mlale JKT kwenye Uwanja wa Samora mjini Iringa wakati KMC itacheza na Coastal Union kwenye Uwanja wa Azam, Dar es Salaam.
    Kundi C kutakuwa na mchezo mmoja ambako Rhino itacheza na JKT Oljoro kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora.
    Ligi Daraja la Pili Tanzania Bara (SDL), inatarajiwa kuanza Septemba 30, mwaka huu kwa timu kuchuana katika viwanja vitano tofauti.
    Kwa mujibu wa Ratiba ambayo imeambatanishwa, michezo ya siku hiyo itakuwa ni kati ya Abajalo na Cosmopolitan; Namungo na Reha kutoka Kundi A wakati kundi B kutakuwa na mchezo kati ya Pepsi na Madini.
    Kundi C kutakuwa na mchezo kati ya Burkinafaso na Ihefu kadhalika Boma itacheza na Mkamba Rangers huku Kundi D likikutanisha timu za Bulyanhulu na Milambo.
    Katika Kundi hilo la D Mchezo kati ya Nyanza FC na Area C uliokuwa ufanyike Septemba 30, 2017 siku ya Jumamosi kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha, sasa utachezwa Oktoba 01, 2017 siku ya Jumapili kwenye Uwanja huo huo.
    Sababu za mabadiliko haya ni kutokana na mchezo kati ya Pepsi FC vs Madini FC kuchezwa tarehe 30.09.2017 katika uwanja huo. Awali mchezo wa Nyanza na Area C ulipangwa kufanyika mkoani Manyara, lakini kutokana na hali ya uwanja ilibidi Bodi ya ligi ufanye mabadiliko husika.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA NA MTIBWA SUGAR SHUGHULI PEVU UHURU KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top