• HABARI MPYA

    Friday, September 29, 2017

    ANCELOTTI AFUKUZWA BAYERN MUNICH BAADA YA 3-0 ZA PSG

    KOCHA Carlo Ancelotti amefukuzwa Bayern Munich baada ya kuwa kazini kwa mwaka mmoja tu, kufuatia kipigo cha mabao 3-0 kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya Jumatano kutoka kwa Paris Saint Germain.
    Bayern, mabingwa wa Ujerumani, mwaka jana chini ya Ancelotti na kila msimu kati ya mitano iliyopita wamekuwa na matokeo mchanganyiko kwenye michuano hiyo.
    Walichapwa 2-0 na Hoffenheim kabla ya kutoa sare ya 2-2 nyumbani na Wolfsburg kwenye Ligi ya Ujerumani, licha ya kuongoza kwa 2-0.
    Katika taarifa yao rasmi, Bayern wamesema kwamba wameachana na kocha huyo mwenye umri wa miaka 58 kufuatia kikao cha ndani baada ya kipigo cha PSG katikati ya wiki.

    Ancelotti akiwasili mjini Munich Alhamisi kutoka Paris ambako Jumatano waliichezea 3-0  za PSG PICHA ZAIDI GONGA HAPA  
    REKODI YA ANCELOTTI BAYERN MUNICH DHIDI YA REKODI YA PEP GUARDIOLA
    AncelottiGuardiola
    60Mechi161
    42Kushinda121
    9Sare21
    9Kufungwa19
    2.6Mabao/mechi2.5
    0.8Mabao ya kufungwa/mechi0.7
    70%Asilimia ya ushindi75%

    Msaidizi wa Ancelotti, Willy Sagnol ataiongoza timu kwa muda, huku kocha wa Hoffenheim, Julian Nagelsmann akipewa nafasi kubwa ya mrithi wa kudumu wa Mtaliano huyo.
    Mtendaji Mkuu, Karl-Heinz Rummenigge wakati huo huo amekuwa na majadiliano binafsi na kipenzi chake, kocha wa zamani wa Borussia Dortmund, Thomas Tuchel na kuna uwezekano kocha huyo akawa Mjerumani wa kwanza kuishika timu hiyo tangu kuondoka kwa Jupp Heynckes mwaka 2013.
    Rummenigge amesema katika taarifa yake kwenye tovuti ya Bayern Munich kwamba: "Kiwango cha timu yetu tangu mwanzo wa msimu hakijafikia matarajio tuliyojiwekea. 
    "Mechi ya Paris ilituonyesha wazi tunapaswa kufanya maamuzi. Hasan Salihamidzic [Mkurugenzi wa Usajili wa Bayern] na mimi tulizungumza na Carlo leo na kumjulisha uamuzi wetu,".
    "Ningependa kumshukuru Carlo kwa ushirikiano wake na ninasikitika kwa hatua hii. Carlo ni rafiki yangu na atabaki kuwa hivyo, lakini tunapaswa kuchukua maamuzi ya kiprofesheno kwa maslahi ya Bayern," amesema. 
    Wanne kati ya wasaidizi wa Ancelotti - Wataliano wenzake, Davide Ancelotti (mtoto wa Carlo), Giovanni Mauri, Francesco Mauri na Mino Fulco - pia wameondoka Bayern. 
    Kocha huyo wa zamani wa Real Madrid na Chelsea, Ancelotti alianza kazi Bayern Julai mwaka 2016 akichukua nafasi ya Mspaniola Pep Guardiola aliyehamia Manchester City.
    Akaendeleza umwamba wa Bayern katika Bundesliga kwa kuiwezesha kubeba ubingwa ikiwa ina pointi 10 zaidi ya washindi wa pili, RB Leipzig. Pia ametwaa mataji ya Super Cup ya Ujerumani msimu huu na uliopita.
    Pamoja na hayo walifungwa 3-2 nyumbani katika Nusu Fainali ya Kombe la Ujerumani na Borussia Dortmund, na kwenye Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa msimu wa 2016-2017 walifungwa na Real Madrid. Bayern haijashinda taji lolote la Ulaya tangu mwaka 2013. 
    Kumekuwa na matatizo pia ndani na nje ya Uwanja - kipa namba moja Manuel Neuer ni majeruhi na ataendelea kuwa nje hadi baada ya Krisimasi na mbadala wake, Sven Ulreich ameshindwa kuziba pengo hilo vizuri, akifanya makosa na kufungwa bao la kwanza la kizembe dhidi ya Wolfsburg.
    Mshambuliaji tegemeo, Robert Lewandowski amelaumu sera ya ubakhili ya klabu akisema wanapaswa kutumia fedha zaidi kusajili huku pia mashabiki na vyombo vya habari wakilaumu Thomas Muller kutokupewa muda wa kutosha wa kucheza.
    Kusajiliwa kwa James Rodriguez kwa mkopo wa miaka miwili kumeleta mawazo tofauti, wakati kustaafu kwa Philipp Lahm na Xabi Alonso kumeuacha uongozi katika wakati mgumu. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ANCELOTTI AFUKUZWA BAYERN MUNICH BAADA YA 3-0 ZA PSG Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top