• HABARI MPYA

    Thursday, September 28, 2017

    NIGERIA KUWASILI DAR USIKU WA LEO KUIVAA TANZANIA JUMAPILI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya soka ya taifa ya wanawake wenye umri wa chini ya miaka 20 ya Nigeria ‘Falconets’ inatarajiwa kutua nchini usiku wa kumkia Ijumaa Septemba 29, mwaka huu.
    Wakitokea Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Nnamdi Azikiwe, ulioko Abuja nchini Nigeria, Falconets watatumia ndege ya Shirika la Ndege la Ethiopia ikiwa ni kikosi cha watu 31 miongoni mwake wako maofisa 13 kuja Dar es Salaam, Tanzania. 
    Timu hiyo ya wanawake yenye wachezaji 18, watatua Dar es Salaam saa 9.40 usiku na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limewapangia kuishi katika Hoteli ya Urban Rose iliyoko katikati ya jiji la Dar es Salaam katika kipindi cha siku tatu watakazokuwa hapa jijini.
    Wanakuja kucheza na timu ya Taifa ya wasichana wenye umri wa chini ya miaka 20 ya Tanzania ‘Tanzanite’ kwenye mchezo wa marudiano kuwania kucheza fainali za Kombe la Dunia. Fainali za Kombe la Dunia zitafanyika Ufaransa hapo mwakani.
    Mchezo huo wa marudiano utafanyika Jumapili Oktoba mosi, mwaka huu kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam kuanzia saa 10.00 jioni.
    Tanzania ina matumaini ya kufanya vema kwenye mchezo huo wa marudio licha ya kupoteza kwa mabao 3-0 katika mchezo wa kwanza uliofanyika Uwanja wa Samwel Oigemudia ulioko Jimbo la Benin, Nigeria.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NIGERIA KUWASILI DAR USIKU WA LEO KUIVAA TANZANIA JUMAPILI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top