• HABARI MPYA

    Sunday, September 24, 2017

    RUVU SHOOTING YAIPUNGUZA KASI MTIBWA SUGAR LIGI KUU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MTIBWA Sugar imepunguzwa kasi katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 na Ruvu Shooting Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.
    Matokeo haya, yanawafanya Mtibwa ifikishe pointi 10 baada ya kucheza mechi nne, lakini haindoki kileleni hata baada ya mecho zote za Raundi hii ya nne, kwani timu zinazofuatia zina pointi nane kila moja.
    Katika mchezo wa leo, bao la Ruvu Shooting lilifungwa na Zuberi Dabi dakika ya kwanza tu, kabla ya Mtibwa Sugar kusawazisha dakika ya 55 kupitia kwa Stahmil Mbonde.
    Mechi nyingine za Ligi Kuu leo, Stand United imepata ushindi wa kwanza, baada ya kuichapa Mbeya City mabao 2-1 katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga.
    Ally Ally aliunawa mpira kwenye boksi kuwapa penalti Mbeya City iliyofungwa na kiungo Mohammed Samatta kuipatia timu hiyo bao la kusawazisha dakika ya 58, baada ya Kisatia Sahani kuifungia Stand United bao la kuongoza dakika ya 51.
    Ally Ally akaibuka shujaa baada ya kupambana na kusawazisha makosa yake na kufanikiwa kuifungia Stand United bao la ushindi dakika ya 62. Mchezo mwingine wa leo, Singida United wameibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Kagera Sugar Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma, bao pekee la Mzimbabwe, Tafadzwa Kutinyu dakika ya 87 kwa penalti.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: RUVU SHOOTING YAIPUNGUZA KASI MTIBWA SUGAR LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top