• HABARI MPYA

    Monday, January 17, 2022

    SIMBA YACHAPWA 1-0 NA MBEYA CITY PUNGUFU SOKOINE

    MABINGWA watetezi, Simba SC wamepoteza mechi ya kwanza ya msimu wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya kuchapwa 1-0 na wenyeji, Mbeya City jioni ya leo Uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya.
    Bao pekee la Mbeya City leo limefungwa na mshambuliaji Paul John Nonga dakika ya 41 akimchambua kwa ustadi kipa namba moja Tanzania, Aishi Salum Manula baada ya kumtoka beki Mkongo, Hennock Inonga Baka 'Varane'.
    Mshambuliaji Mkongo, Chris Kope Mutshimba Mugalu aligongesha mwamba wa mkwaju wa penalti dakika ya na Nahodha, John Raphael Bocco alipojaribu kwenda kumalizia ndani ya sita, kipa Deogratius Munishi 'Dida' alidaka.
    Penalti hiyo ilitolewa baada ya beki Juma Shemhuni kuangukia mpira wakati akijaribu kuokoa shambulizi la winga wa Simba, Kibu Dennis.
    Kwa zaidi ya nusu ya mchezo huo, Mbeya City ilicheza pungufu baada ya beki wake, Mpoki Mwakinyuke kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 43 kufuatia kuonyeshwa kadi ya pili ya njano.
    Kwa ushindi huo, Mbeya City inafikisha pointi 19 baada ya mechi 12 na kusogea nafasi ya tatu, ikizidiwa poniti tano na Simba ambayo imecheza mechi 11 - wote wakiwa nyuma ya Yanga wenye pointi 32 za mechi 12.
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, Polisi Tanzania wamelazimishwa sare ya bila kufungana na Namungo FC Uwanja wa Ushirika mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.
    Polisi sasa ina pointi 18 katika nafasi ya nne na Namungo wamefikisha pointi 14 katika nafasi ya nane baada ya timu zote kucheza mechi 12.
     
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YACHAPWA 1-0 NA MBEYA CITY PUNGUFU SOKOINE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top