• HABARI MPYA

    Thursday, January 24, 2019

    ISMAILIA YA YAHYA ZAYD YAENGULIWA LIGI YA MABINGWA AFRIKA

    Na Mwandishi Wetu, CAIRO
    TIMU ya Ismailia ya Misri anayochezwa mshambuliaji chipukizi Mtanzania, Yahya Zayd imeenguliwa kwenye orodha ya timu za Kundi C Ligi ya Mabingwa Afrika.
    Shirikisho la Soka Afrika (CAF) limetangaza hayo jana likisema kwamba limeichukulia hatua hiyo Ismailia baada ya mashabiki wake kufanya fujo mwishoni mwa mchezo dhidi ya Club Africain mjini Ismailia.
    Refa wa mchezo huo, Neant Alioum alilazimika kusitisha mchezo huo baina ya Ismailia na Club Africain dakika za mwishoni kutokana na vurugu za mashabiki wa wenyeji, ambao walikuwa wanapingana na maamuzi ya marefa.

    Yahya Zayd timu yake, Ismailia ya Misri imeenguliwa kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika

    Na vurugu hizo zilitokea wakati Club Africain ipo mbele kwa mabao 2-1 kabla ya waamuzi kuivunja mashabiki wa Ismailia kuanza kuwarushia mawe na chupa za maji marefa na wachezaji wa wageni kuanzia dakika ya 86.
    Baada ya hatua hiyo matokeo yote ya Ismailia katika mechi za Kundi C yanafutwa na kundi hilo sasa linabaki na timu tatu ambazo ni CS Constantine ya Algeria, Club Africain na TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Zayd amejiunga na Ismailia mwezi huu akitokea Azam FC ya nyumbani na anakwenda kuwa mchezaji wa pili wa Tanzania katika Ligi Kuu ya Misri baada ya Himid Mao. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ISMAILIA YA YAHYA ZAYD YAENGULIWA LIGI YA MABINGWA AFRIKA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top