• HABARI MPYA

    Wednesday, January 23, 2019

    SPORTPESA CUP; MBAO FC YAWANG’OA KWA MATUTA MABINGWA WATETEZI GOR

    Na Sada Salmin, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Mbao FC imefanikiwa kwenda Nusu Fainali ya michuano ya SportPesa Super Cup baada ya ushindi wa penalti 4-3 kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 90 na mabingwa watetezi, Gor Mahia ya Kenya jioni ya leo uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Waliofunga penalti za Mbao FC, timu kutoka mjini Mwanza inayofundishwa na kipa wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Ally Bushiri ni Said Khamis, Abubakar Ngalema, Hamim Abdukarim na David Mwasa, wakati ibrahim Hashim alikosa.
    Kwa upande wa Gor Mahia, moja ya timu zinazoshiriki hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika waliofunga ni Francis Kahata, Jaqcue Tuyisenge na Boniface Omondi, wakati Harun Shakava na Shafiq Batambuze walikosa.
    Abubakar Ngalema akikimbia kushangilia baada ya kuifungia Mbao FC bao la kusawazisha leo 
    Mchezaji wa Mbao FC, Ibrahim Hashim akikabidhiwa tuzo ya Mchezaji Bora wa Mechi
    Wachezaji wa Mbao FC wakishangilia ushindi wao baada ya mchezo

    Katika mchezo huo ulioanza Saa 8:15 mchana, Gor Mahia walitangulia kwa bao la mkwaju wa penalti lililofungwa na Denis Oliech dakika ya 51 kufuatia beki wa Mbao FC, Amos Charles kuunawa mpira kwenye boksi.
    Mbao FC ikasawazisdha bao hilo dakika ya 71 kupitia kwa mchezaji wake hodari, Abubakar Ngalema na kuuhamishia mchezo huo kwenye matuta ambako wamefanikiwa kuwavua taji mabingwa mara zote wa michuano hiyo miaka miwili mfululizo iliyopita, Gor Mahia na kwenda Nusu Fainali.
    Mbao sasa itakutana na ushindi kati ya Simba SC ya Dar es Salaam na AFC Leopards ya Kenya katika Nusu Fainali mwishoni mwa wiki. 
    Kikosi cha Mbao FC kilikuwa: Metacha Mnata, Vicent Philipo, Amos Charles, David Mwasa, Erick Mulilo, Said Khamis, Ibrahim Hashim, Gervas Rambo/Abubakar Ngalema dk63, Pastor Athanas/Rejesh Kotecha dk 78 na Hamimu Abdukarim
    Gor Mahia: Fredrick Odhiambo, Philemon Otieno, Geoffrey Ochieng/Shafiq Batambuze dk45, Joash Onyango/Jacques Tuyisenge dk 84, Haruna Shakavah, Cercidy Okeyo, Lawrence Juma, Denis Oliech/Francis Mustafa dk65, Erisa Ssekisambu na George Odhiambo/Boniface Omondi dk46.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SPORTPESA CUP; MBAO FC YAWANG’OA KWA MATUTA MABINGWA WATETEZI GOR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top