• HABARI MPYA

    Thursday, January 17, 2019

    KMC YAITANDIKA COASTAL UNION 5-2 NA KUKALIA NAFASI YA SIMBA SC LIGI KUU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni (KMC) imeibuka na ushindi wa mabao 5-2 dhidi ya Coastal Union ya Tanga katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.
    Ushindi huo mnono kwa timu hiyo ya kocha Mrundi, Etienne Ndayiragijje unaifanya KMC ifikishe pointi 34 baada ya kucheza mechi 22 na kupanda hadi nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu, sasa ikiwazidi kwa pointi mabingwa watetezi, SImba SC ambao hata hivyo wamecheza mechi 14 tu. 
    KMC sasa inazidiwa pointi 20 na Yanga SC wanaoongoza Ligi Kuu wakiwa wamecheza mechi 19 na wanafuatiwa na Azam FC wenye pointi 41 za mechi 18.
    Wachezaji wa KMC wakipongezana baada ya kazi nzuri leo Uwanja wa Uhuru 

    Ally Msengi wa KMC akiwatoka wachezaji wa Coastal Union leo Uwanja wa Uhuru
    Ally Msengi akitafuta maarifa ya kupasua katikati ya wachezaji wa Coastal Union 

    Ally Msengi akipiga mpira dhidi ya kipa wa Coastal Union, Hussein Sharrif 'Casillas'

    Coastal Union inayofundishwa na mchezaji wake wa zamani, Juma Mgunda inabaki na pointi zake 25 baada ya kucheza mechi 21 na kuendelea kushika nafasi ya 10 kwenye Ligi Kuu ya timu 20. 
    Katika mchezo wa leo, mabao ya KMC yamefungwa na Charles Ilamfya dakika ya 15, Ally Msengi dakika ya 21, Emmanuel Mvuyekure dakika ya 75, Elias Maguri dakika ya 86 na Cliff Buyoya dakika ya 90 na ushei, wakati ya Coastal Union yote yamefungwa na Ayoub Lyanga dakika za 69 na 78.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KMC YAITANDIKA COASTAL UNION 5-2 NA KUKALIA NAFASI YA SIMBA SC LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top