• HABARI MPYA

    Sunday, January 27, 2019

    NI KARIOBANGI SHARKS MABINGWA WAPYA WA SPORTPESA SUPER CUP 2018

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Kariobangi Sharks imefanikiwa kutwaa ubingwa wa michuano ya SportPesa Super Cup baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya Bandari, zote za Kenya katika mchezo mzuri wa fainali uliofanyika Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam jioni ya leo.
    Pongezi kwa mfungaji wa bao pekee la ushindi Mwendwa Harrison dakika ya 61 na kwa ushindi huo, Kariobangi Sharks ya Nairobi wamezawadiwa dola za Kimarekani 30,000, zaidi ya Sh. Milioni 65 za Tanzania na pia watamenyana na klabu ya Everton ya Uingereza.
    Bandari kutoka Mombasa inayofundishwa na mchezaji wa zamani wa Yanga SC, Ben Mwalala yenyewe imepatiwa dola 10,000 za Kimarekani zaidi ya Sh. Milioni 22 za Tanzania kwa kumaliza nafasi ya pili.

    Washindi wa tatu, Simba SC ambao wameifunga Mbao FC kwa penalti 5-3 baada ya sare ya 0-0 ndani ya dakika 90, wamepatiwa dola 7,500, zaidi ya Sh. Milioni 18 za Tanzania.
    Mbao FC wamepata dola 5,000, zaidi ya Sh. Milioni 12 za Tanzania na washiriki wengine wote, AFC Leopards, Gor Mahia na Yanga SC wamepatiwa sola 2,500 kila mmoja, zaidi ya Sh. Milioni 6 za hapa.
    Harrison Mwendwa pia akachaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Mechi baada ya kuisaidia timu yake kutwaa ubingwa wa michuano hiyo kwa kupachika bao pekee la ushindi.
    Wakenya wamekuwa wakitamba kwenye michuano hiyo tangu ianzishwe, mwaka 2017 Gor Mahia wakiwafunga mahaimu wao, AFC Leopards 3-0 Uwanja wa Taifa wa Dar es Salaam na mwaka jana wakiwafunga Simba SC 2-1 Uwanja wa Afraha mjini Nakuru.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NI KARIOBANGI SHARKS MABINGWA WAPYA WA SPORTPESA SUPER CUP 2018 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top