• HABARI MPYA

    Wednesday, July 26, 2023

    WIZARA YA MICHEZO YAKUTANA NA MARAIS WA NCHI WANACHAMA CECAFA DAR


    KATIBU Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Saidi Yakubu amekutana na Marais wa Mashirikisho ya Mpira wa Miguu ya nchi wanachama wa Shirikisho la Mpira wa Miguu la nchi za Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) ambapo amewaomba kuiunga mkono Tanzania, Kenya na Uganda ambazo  zinaomba kuwa mwenyeji wa Mashindano ya Shirikisho la Mpira wa  Miguu Afrika (CAF) 2027.
    Marais walioshiriki kikao hicho ni Wales Karia, Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ambaye ni Rais wa CECAFA sasa,  Augustino Maduot, Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Sudan Kusini, Paulos Andromariam, Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Eritrea, Isayas Jiral, Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Ethiopia, Doris Petra Mwakilishi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Kenya pamoja na watendaji wakuu wa CECAFA Bw. Mossi Yusuf Meneja wa Mashindano CECAFA na Auka Gocheo Mkurugenzi Mtendaji wa CECAFA.
    Kikao hicho  kimefanyika kabla ya mechi ya ufunguzi kati ya Tanzania na Burundi ambayo imechezwa Julai 25, 2023 katika Uwanja wa Azam Chamazi jijini Dar es salaam kwa wasichana U- 18 ambapo wamejadili namna bora ya kufanikisha azma hiyo kwa kwa ukanda wa Afrika Mashariki.
    Viongozi hao wamemuahidi Katibu Mkuu ushirikiano wakati wote wa maandalizi na wakati wa michuano hiyo ya Afrika endapo Tanzania, Kenya na Uganda zitapewa dhamana ya kuandaa michuano hayo.
    Hadi kipenga cha mwisho,  timu ya Wasichana U-18 ya Tanzania imeibuka kidedea kwa kuwafunga wenzao wa Burundi kwa magoli 3-0 ikiwa ni  mechi ya ufunguzi wa michuano CECAFA.
    Magoli ya Tanzania yamefungwa na Winfrida Gerald jezi Na 7 ambaye alifunga goli la kwanza, Sarah Joel jezi Na 19 alifunga goli la pili huku goli la tatu likifungwa na Aisha Juma jezi Na 9.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WIZARA YA MICHEZO YAKUTANA NA MARAIS WA NCHI WANACHAMA CECAFA DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top