• HABARI MPYA

    Friday, July 21, 2023

    KOCHA MPYA YANGA AAHIDI SOKA YA KUVUTIA DHIDI YA KAIZER CHIEFS KESHO


    KOCHA mpya wa Yanga SC, Muargentina Miguel Angel Gamondi ameahidi mchezo wa kuvutia kesho katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini kwenye Kilele cha Wiki ya Mwananchi Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Akizungumza leo kwenye mkutano na Waandishi wa Habari Jijini Dar es Salaam, Gamondi amesema kwamba watajaribu kucheza vizuri ili kuwapa furaha mashabiki.
    "Tunatarajia kuwa na malengo makubwa zaidi kwa sababu hii ni klabu kubwa yenye mashabiki wengi wenye nguvu na ushawishi kutaka klabu hii iendelee kufanya vizuri zaidi hasa kwenye mashindano ya kimataifa," amesema Gamondi.
    Gamondi kwa upande wa timu bado wapo kwenye maandalizi na mchezo wa kesho dhidi ya Kaizer Chiefs watautumia kama sehemu ya maandalizi yao kuelekea msimu mpya.  
    "Kesho ni siku kubwa kwa mashabiki wa Yanga pamoja na sisi wote tunakwenda kupata nafasi ya kusherehekea kufunguliwa kwa msimu huu mpya tukiwa na matarajio ya kuendelea kuipambania klabu hii kubwa yenye historia kubwa,"ameongeza Gamondi.


    Kwa upande wake winga mpya wa timu hiyo aliyesajiliwa kutoka Marumo Gallants ya Afrika Kusini, Skudu Mahlatse Makudubela amewataka mashabiki wa Yanga kujitokeza kwa wingi Uwanja wa Mkapa kwani watawapa burudani nzuri.
    "Tupo kwenye maandalizi ya awali kujiandaa na msimu mpya, kwa niaba ya wachezaji wenzangu kwanza niseme ni heshima kubwa sana kwangu kuwawakilisha kwenye mkutano huu na ujumbe wetu kwenu tunaomba kesho mje kwa wingi tumewaandalia burudani nzuri,"amesema Mahlatse. 
    Kilele cha Wiki ya Mwananchi ni siku maalum ambayo Yanga hutumia kutambulisha kikosi chake kizima cha msimu pamoja na benchi la Ufundi kabla ya mchezo maalum wa kirafiki, ambayo yote hutanguliwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KOCHA MPYA YANGA AAHIDI SOKA YA KUVUTIA DHIDI YA KAIZER CHIEFS KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top