• HABARI MPYA

    Sunday, August 08, 2021

    YANGA SC YAMSAJILI KIPA WA KIMATAIFA WA MALI ALIYEWEZESHA NCHI YAKE KUSHIKA NAFASI YA TATU KOMBE LA DUNIA LA U20

     KLABU ya Yanga SC imemtambulisha kipa wa kimataifa Mali, Djigui Diarra kuwa mchezaji wake mpya kutoka Stade Malien ya kwao, Bamako.
    Diarra anakuwa mchezaji mpya wa nne kutambulishwa Yanga na mgeni wa tatu baada ya washambuliaji Wakongo, Fiston Mayele kutoka AS Vita ya kwao, Kinshasa na Heritier Makambo kutoka Horoya ya Guinea pamoja na mzawa, Yussuf Athumani, mshambuliaji pia kutoka Biashara United ya Mara.
    Diarra mwenye umri wa miaka 26 ana uzoefu wa kutosha kimataifa, kwani pamoja na kuingia Stade Malien mwaka 2011 pia amecheza mashindano kadhaa makubwa, zikiwemo Fainali za Kombe la Dunia za U20 mwaka 2015 Mali ikimaliza nafasi ya tatu.


    Lakini pia alikuwemo kwenye kikosi cha U23 ya Mali kwenye Fainali za Afrika mwaka 2015 kabla ya kupandishwa rasmi timu ya wakubwa mwaka 2016.
    Alikuwa kipa wa kwanza wa Mali kwenye Fainali za CHAN mwaka 2016 nchini Rwanda alipoiwezesha timu hiyo kushika nafasi ya pili baada ya kufungwa mabao 3-0 na DRC kwenye fainali. Diarra ambaye anasifika kwa kuokoa mikwaju ya penalti, aliteuliwa kwenye kikosi bora cha CHAN 2016 kama kipa wa akiba.
    Ameshinda mataji manne ya Ligi Kuu ya Mali akiwa na Stade Malien misimu ya 2012–2013, 2013–2014, 2014–2015 na 2015–2016 pamoja na Kombe la FA ya nchi hiyo mara mbili 2013 na 2015 na Super Cup ya nchini humo 2014 na 2015.
    Aliteuliwa pia kwenye Timu ya Mwaka 2015 ya CAF na ni mshindi wa Tuzo ya Mchezaji Bora wa Mwaka wa Mali msimu wa 2014–2015.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YAMSAJILI KIPA WA KIMATAIFA WA MALI ALIYEWEZESHA NCHI YAKE KUSHIKA NAFASI YA TATU KOMBE LA DUNIA LA U20 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top