• HABARI MPYA

    Sunday, August 23, 2015

    SIMBA WANA FEDHA ZA OKWI, KWA NINI WATAFUTE WACHEZAJI WA ‘BEI POA’?

    MWEZI uliopita klabu ya Simba SC ilimuuza mshambuliaji wake mahiri, Mganda Emmanuel Arnold Okwi klabu ya SonderjyskE FC ya Ligi Kuu ya Denmark kwa dola za Kimarekani 110,000 (Sh. 250).
    Okwi aliyesaini Mkataba wa miaka mitano tayari ameanza kazi Haderslev na sasa Simba SC wanatafuta mbadala wake na inaonekana wanatafuta mchezaji wa kiwango chake.
    Mwishoni mwa wiki iliyopita Simba SC ilimtumia katika mchezo wa kirafiki mshambuliaji Mrundi, Kevin Ndayisenga akacheza vizuri na kufunga bao timu hiyo ikishinda 2-1 dhidi ya URA ya Uganda Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 
    Lakini Ijumaa usiku Ndayisenga amepanda ndege kurejea kwao Burundi baada ya Simba SC kushindwa kufika gharama za manunuzi yake, ambayo si zaidi ya dola 50,000 jumla kwa gharama halisi (Sh. Milioni 100)
    Kuondoka kwa Ndayisenga kumewasikitisha mno wana Simba SC, kwani mchezaji huyo aliwasisimua mashabiki wa timu hiyo ya Msimbazi kwa soka yake nzuri na kuanza kutamba wamepata ‘kifaa’ cha kuwaadabisha wapinzani.
    Ikumbukwe, Ndayisenga alikuwa mpango mbadala baada ya Simba SC kumkosa mshambuliaji mwingine hatari wa Vital’O, Laudit Mavugo kufuatia klabu mbili za Burundi kupandisha thamani ya mchezaji huyo na kuwa Sh. Milioni 200, badala 110 walizokubaliana awali.
    Aidha, kuibuka pia kwa mzozo mpya kati ya klabu ya Vital’O FC na Solidarity FC, inayodai kumlea Mavugo na kudai ina hakimiliki ya mchezaji huyo nako kuliishitua Simba.
    Vital’O ikaikoroga zaidi Simba SC baada ya kudai kiwepo kipengele cha wao kupata asilimia 50 kama mchezaji huyo atauzwa na Wekundu hao wa Msimbazi kwenda klabu nyingine.   
    Kidogo kwa Mavugo unaweza kuelewa, kwamba ingekuwa vigumu kwa Simba SC kununua mchezaji kutoka nchi jirani kwa gharama sawa na iliyouzia mchezaji wake Ulaya.
    Lakini bado thamani ya mchezaji haitazamwi kwa nchi anayotoka, bali kwa uwezo wake kiuchezaji, umri na utimamu wake wa mwili na afya.
    Hivyo Simba SC ingeweza kumnunua Mavugo hata kwa gharama zaidi ya ilizomuuza Okwi Ulaya, iwapo tu ingejiridhisha ni mchezaji mzuri, yuko fiti kikamilifu na ni kijana mdogo, ambaye nayo inaweza kumuuza kwa bei kubwa zaidi popote baadaye.
    Kuhusu Ndayisenga, alionekana ni kijana mdogo na aliyekamilika- ambaye klabu kama Simba SC kutoa dola 50,000 jumla kumnunua isingekuwa vibaya.
    Hata hivyo, ikiwa na dola 110,000 kwenye akaunti yake baada ya kumuuza Okwi, Simba SC imeshindwa kutoa nusu ya fedha hizo kumnunua Ndayisenga.
    Siku mbii baada ya kuondoka Ndayisenga, Simba SC wameleta mshambuliaji mwingine, Msenegali, Papa Niang kwa ajili ya majaribio kutoka klabu ya Alianza F.C. ya El Salvador ambaye ni mdogo wa mshambuliaji wa kimataifa wa zamani wa Senegal, Mamadou Niang.
    Mchezaji huyo aliyewahi kuchezea timu za CF Mounana ya Gabon, Al Shabab SC ya Kuwait, FC Vostok ya Kazakhstan, FF Jaro, AC Oulu na FC OPA za Finland kesho anatarajiwa kuichezea Simba SC katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Mwadui Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Mchezaji mzuri unaweza ukamjua hata anapocheza na timu ya kiwango cha chini, lakini inapendeza ukamjaribu mchezaji katika mechi ngumu, kipimo ambacho Ndayisenga alikipata mbele ya mabeki wa URA.
    Wachambuzi mbalimbali wa soka nchini na makocha walisifu uchezaji wa Ndayisenga, ana nguvu, kasi, uwezo wa kumiliki mpira, kucheza na timu, kufunga na kutengeneza nafasi za wengine kufunga baada ya mechi na URA.
    Na kwa sababu tunafahamu Uganda imetuzidi kisoka, kipimo cha URA kilikuwa kizuri mno kwa mchezaji huyo na Simba SC kwa ujumla kama timu.
    Narudia, mchezaji mzuri unaweza kumjua hata anapocheza dhidi ya wachezaji wa kiwango cha chini yake- hivyo hata mechi dhidi ya Mwadui inaweza kusaidia kuujua uwezo wa Niang, lakini tu kwa Ndayisenga Simba SC imeacha mchezaji mzuri.
    Naamini baada ya kumuuza Okwi, mchezaji ambaye alikuwa ana vitu vya ziada- suala lilikuwa ni Simba SC kumpata mchezaji mwingine wa ubora wa Mganda huyo.
    Hamisi Kiiza ni mzuri, lakini si wa kiwango cha Mganda mwenzake huyo na ndiyo maana Simba SC bado wanahangaika.
    Wasiwasi tu ni kwamba, Simba SC inaonekana haiko tayari kutumia japo nusu ya fedha ilizopata kwa mauzo ya Okwi kumnunua mchezaji mwingine wa kiwango hicho.
    Ndayisenga alikuwa mchezaji huru na zaidi ya dau la yeye kusaini na malipo ya wakala wake- ambazo zote zisingezaidi dola za Kimarekani 50,000 hakukuwa na gharama nyingine, lakini Simba SC imeshindwa.
    Sasa amekuja Niang na kesho atacheza mbele ya maelfu ya mashabiki wa Simba SC katika mechi laini dhidi ya Mwadui FC iliyopanda Ligi Kuu msimu huu.
    Dhahiri kama mchezaji huyo atashangiliwa kesho, kitakachofuata ni mazungumzo ya biashara mezani baina ya Simba na wakala wake. 
    Mchezaji kutoka Magharibi mwa Afrika, tusitarajie dau lake linaweza kuwa chini ya dola 50,000 zile zile ambazo Simba SC imeshindwa kutoa kumnunua Ndayisenga, tutarajie nini hapo?
    Viongozi wa Simba SC wanapaswa kufahamu kwamba wanatakiwa kumkamilishia kocha Muingereza Dylan Kerr wachezaji ili aanze rasmi kuandaa timu kwa ajili ya Ligi Kuu.
    Na kwa staili hii Simba SC wanaweza kujikuta wanaacha mchezaji mzuri, mwisho wa siku wakasajili galasa na kuzidi kujiwekea mazingira magumu ya kushindana na Yanga na Azam FC katika mbio za ubingwa.
    Nashangaa Simba SC hadi sasa hawajajifunza gharama za wachezaji wa bei rahisi baada ya yaliyowatokea kwa Paul Kiongera, waliposajili majeruhi sugu.
    Nataka niwaambie kitu kimoja Simba SC leo; waache mzaha, watumie nusu ya fedha walizopata kwa mauzo ya Okwi, kununua mchezaji mwingine bora kama wanataka mrithi wa Mganda huyo. Jumapili njema. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA WANA FEDHA ZA OKWI, KWA NINI WATAFUTE WACHEZAJI WA ‘BEI POA’? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top