• HABARI MPYA

    Monday, August 24, 2015

    TP MAZEMBE ‘YAADABISHWA’ SUDAN, YAPIGWA 1-0 NA HILAL, MERREIKH YATINGA NUSU FAINALI

    Kikosi cha Mazembe kilichofungwa 1-0 na El Hilal jana
    TP Mazembe imepunguzwa kasi kwa kichapo cha bao 1-0 mbele ya wenyeji, El Hilal ya Sudan katika mchezo wa Kundi A Ligi ya Mabingwa Afrika usiku wa jana. 
    Matokeo hayo yanaifanya Hilal ifikishe pointi nane sawa na Mazembe na kufungana kileleni, kutokana na kulingana pia kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.
    Moghreb Tetouan ya Morocco nayo imefikisha pointi nane pia baada ya ushindi wa 2-1 jana dhidi ya Smouha ya Misri, inayoendelea kushika mkia kwa pointi zake tatu.
    Katika mechi za Kundi B juzi El Merreikh ya Sudan ilipata ushindi wa ugenini wa mabao 3-2 dhidi ya wenyeji MC Eulma nchini Algeria, wakati Ijumaa 
    USM Alger iliyawafunga ndugu zao ES Setif zote za Algeria mabao 3-0.
    Kwa matokeo hayo, USM Alger inafikisha pointi 15 na kuendelea kushika usukani wa Kundi B, ikifuatiwa na Merreikh yenye pointi 10 sasa, ES Setif pointi nne, wakati MC Eulma haina pointi inashika mkiwa baada ya kufungwa mechi zote tano.
    Mechi za makundi zitahitimishwa Septemba 12, Smouha wakiikaribisha El Hilal na TP Mazembe wakiwa wenyeji wa Moghreb Tetouan huku Kundi B, Merreikh iliyoitoa Azam FC katika Raundi ya kwanza kwa jumla ya 3-2 baada ya kufungwa 2-0 Dar es Salaam na kushinda 3-0 Sudan ikiikaribisha USM Alger na ES Setif wakimenyana na Waalgeria wenzao, MC Eulma.
    Timu mbili za juu kila kundi zitakwenda Nusu Fainali na mchakato unaonekana kuwa mkali zaidi kwa Kundi A, ambalo timu tatu zinachuana huku Kundi B, tayari Merreikh na USM Alger zimefuzu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TP MAZEMBE ‘YAADABISHWA’ SUDAN, YAPIGWA 1-0 NA HILAL, MERREIKH YATINGA NUSU FAINALI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top