• HABARI MPYA

    Monday, August 24, 2015

    KADO AKIMBIZWA HOSPITALI BAADA YA KUZIMIA UWANJANI SIMBA IKITOKA SARE NA MWADUI FC

    Kipa Shaaban Hassan Kado akipatiwa huduma ya kwanza katika zahanati ndogo ya Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kabla ya kukimbizwa hospitali kufuatia kupoteza fahamu katika mchezo dhidi ya Simba SC leo
    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KIPA bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu uliopita, Shaaban Hassan Kado wa Mwadui FC ya Shinyanga amekimbizwa hospitali baada ya kuzimia katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Simba SC uliomalizika kwa sare ya 0-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jioni ya leo.
    Kado ambaye msimu uliopita alidakia Coastal Union ya Tanga, aliumia dakika ya 77 baada ya kugongana na mchezaji mwenzake wakati wa purukushani kwenye lango la Mwadui na nafasi yake ikachukuliwa na Jackson Abdulrahman.
    Mshambuliaji aliye majaribio Simba SC, Msenegali Papa Niang hakuweza kuwashawishi mashabiki leo baada ya kucheza kwa kiwango cha chini.
    Mdogo huyo wa mshambuliaji wa zamani wa kimataifa wa Senegal, Mamadou Niang alionekana anajua mpira, lakini hayuko fiti kabisa kiasi cha kuonekana kutopenda kukaa na mpira.
    Nahodha wa Simba SC, Mussa Hassan Mgosi akimtoka beki wa Mwadui Fc, Joram Mgeveke
    Beki wa Simba SC, Hassan Kessy (kushoto) akimtoka beki wa Mwadui FC, Juma Mnyassa
    Mshambuliaji aliye katika majaribio, Papa Niang (kushoto) akitafuta maarifa ya kumtoka Juma Mnyassa
    Kiungo wa Simba SC, Mwinyi Kazimoto akimtoka Juma Mnyassa wa Mwadui FC 

    Alipewa pasi nyingi na akawa anazigawa haraka na hata aipowekewa mipira kwenye njia hakuwea kumtoka beki yoyote wa Mwadui FC.
    Nahodha Mussa Hassan Mgosi alicheza vizuri sana leo, lakini akashindwa kufunga. 
    Dakika 30 za kwanza Simba walifanya mashambulizi kadhaa katika lango la Mwadui lakini washambuliaji wake hawakuwa makini na kupoteza nafasi.
    Dakika ya pili Simon Sserunkuma alipiga nje akiwa jirani na lango la Mwadui na kupoteza krosi aliyopelekewa na Hassan Kessy.
    Mwadui walijibu shambulizi hilo, lakini Julius Mrope ambaye aliwahi kucheza Simba alichelewa kuunganisha krosi ya Paul Nonga na kupoteza nafasi ya kuifungia timu yake bao katika dakika ya pili.
    Dakika ya 85 kiungo wa zamani wa Simba SC, Jabir Aziz Stima alitaka kuiadhibu timu yake hiyo ya zamani baada ya kufumua shuti kali akiwa nje ya boksi, lakini kipa Peter Manyika akaokoa.
    Kikosi cha Simba SC leo kilikuwa; Vincent Angban/Dennis Richard dk30/Manyika Peter dk65, Hassan Kessy/Issa Ngoa dk65, Emery Nimubona/Samih Nuhu dk46, Juuko Murushid/Peter Mwalyanzi dk46, Said Issa, Justuce Majabvi, Simon Sserunkuma/Joseph Kimwaga dk46, Mwinyi Kazimoto, Awadh Juma, Papa Niang/Danny Lyanga dk46 na Mussa Mgosi/Hamisi Kiiza dk46. 
    Mwadui FC: Shabani Kado/Jackson Abdulrahman dk77, Malika Ndeule, Juma Mnyassa, Iddy Mobby, Joram Mgoveke, Emmanuel Simwanza, Julius Mrope, Jabir Aziz, Paul Nonga/Jerry Tegete dk72, Kelvin Sabato/Nizar Khalfan dk74na Salim Khamis/Fabian Gwasse dk51.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KADO AKIMBIZWA HOSPITALI BAADA YA KUZIMIA UWANJANI SIMBA IKITOKA SARE NA MWADUI FC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top