• HABARI MPYA

    Friday, June 22, 2018

    TFF YATAMBULISHA MFUMO MPYA WA USAJILI LIGI KUU, DARAJA LA KWANZA...KLABU ZOTE KUPEWA SEMINA

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limetambulisha mfumo mpya wa usajili ujulikanao kama TFF FIFA CONNECT baada ya kufungua rasmi dirisha la Usajili kwa klabu za Ligi Kuu, Daraja la Kwanza na Daraja la Pili msimu wa 2018/2019 Juni 15, mwaka huu 2018
    Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano cha TFF, Clifford Ndimbo amesema kwamba baada ya dirisha kufungwa Julai 26,2018, kutakuwa na wiki moja ya pingamizi kuanzia Julai 27 ikifuatiwa na Kamati ya Katiba, Sheria na Hadhi za Wachezaji kukaa kupitisha usajili. 
    Ndimbo amesema kwa kuanzia kutakuwa na mafunzo ya mfumo mpya wa usajili kwa klabu za Ligi Kuu, Daraja la Kwanza na Daraja la Pili yatakayoanza Jumatatu ya Juni 25 makao makuu ya TFF.
    Hakutakuwa na nafasi nyingine ya mafunzo baada ya mafunzo hayo yatakayofanyika kwa siku moja kwa kila Ligi yakianza na klabu za Ligi Kuu Jumatatu Juni 25,2018.
    Kutokana na Changamoto za utumiaji mfumo huo TFF itaendesha mafunzo hayo kwa siku hizo tajwa ili kuhakikisha ufanisi mkubwa katika usajili wa msimu huo mpya.


    Mkuu wa Kitengo cha Habari cha TFF, Clifford Ndimbo akizungumza na Waandishi wa Habari leo 

    Wakati huo huo: Mchakato wa upigaji kura kwa Mchezaji Bora wa Ligi ya Vodacom Tanzania Bara 2017/2018 zoezi la upigaji kura limefungwa Jumatano.
    Zoezi hilo la kupiga kura limehusisha Makocha wa klabu za Ligi Kuu,Manahodha na Wahariri wa Habari za Michezo.
    Wachezaji watatu watakaowania tuzo ya mchezaji bora wa VPL ni Emmanuel Okwi, John Bocco na Erasto Nyoni wote wa Simba.
    Pia kamati imekamilisha uteuzi wa wachezaji watakaowania tuzo katika kategori mbalimbali kwenye sherehe hizo za Tuzo ya Mchezaji Bora wa VPL itakayofanyika ukumbi wa Mlimani, City Dar es Salaam kesho Jumamosi Juni 23 mwaka huu.
    Tuzo 16 zinatarajiwa kutolewa siku hiyo, ambapo baadhi ni za kikanuni za Ligi Kuu Tanzania Bara, ambazo tayari washindi wake wamefahamika, ambazo ni bingwa, mshindi wa pili, mshindi wa tatu, mshindi wa nne na mfungaji bora.
    Ukiacha hizo tano za kikanuni, zipo tuzo 10 ambazo zimefanyiwa kazi na Kamati ya Tuzo kulingana na takwimu mbalimbali za ligi hiyo, ambapo tuzo moja nyingine ya Mchezaji Bora chini ya umri wa miaka 20 (Tuzo ya Ismail Khalfan), inayohusisha vikosi vya vijana vya timu za Ligi Kuu yenyewe inaendelea kufanyiwa kazi kwa vile mashindano yanaendelea mkoani Dodoma na itakapokamilika watatangazwa wateule watatu.
    Tuzo nyingine zitakazotolewa siku hiyo ni Timu yenye Nidhamu inayowaniwa na Kagera Sugar, Simba na Mtibwa Sugar, wakati Mchezaji Bora Chipukizi inawaniwa na Shaaban Idd Chilunda, Yahya Zayd (Azam) na Habibu Kiyombo (Mbao).
    Mwamuzi Msaidizi Bora inawaniwa na Helen Mduma, Mohammed Mkono na Ferdinand Chacha, wakati Mwamuzi Bora wateule ni Elly Sasii, Jonesia Rukyaa na Hans Mabena.
    Tuzo ya Kipa Bora wanaowania ni Aron Kalambo (Prisons), Aishi Manula (Simba) na Razack Abalora (Azam), huku Kocha Bora wateule ni Abdallah Mohamed (Prisons), Zuberi Katwila (Mtibwa) na Pierre Lechantre (Simba).
    Goli Bora ni Seif Karihe (Lipuli) na Shaaban Idd Chilunda (Azam) ambaye ameingiza mabao mawili.
    Tuzo nyingine ambazo zitatolewa Juni 23 ni Mchezaji wa Heshima ambayo licha ya kuwa kamati ina majina ya wachezaji mbalimbali inaoona wanastahili tuzo kwa mwaka husika, lakini haitangazi majina hayo, isipokuwa hutaja jina la aliyepewa tuzo siku ya sherehe. 
    Pia kutakuwa na kikosi bora (VPL Best Eleven), ambacho kitatangazwa siku ya sherehe.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TFF YATAMBULISHA MFUMO MPYA WA USAJILI LIGI KUU, DARAJA LA KWANZA...KLABU ZOTE KUPEWA SEMINA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top