• HABARI MPYA

    Tuesday, June 19, 2018

    SINGIDA UNITED WACHUKUA NAFASI YA YANGA KOMBE LA KAGAME, SIMBA KUFUNGUA DIMBA NA WASOMALI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Singida United imepewa nafasi ya Yanga SC katika michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Kagame Cup inayotarajiwa kuanza Juni 29 hadi Julai 13 mwaka huu mjini Dar es Salaam.
    Hiyo ni kufuatia mabingwa hao mara tano wa michuano hiyo, Yanga SC kujitoa kwa sababu wanakabiliwa na michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.
    Sasa Kundi C litakuwa na timu za Singida United, Simba SC, APR ya Rwanda na Dakadaha ya Somalia, wakati Kundi  A linabaki na timu za Azam FC ya Dar es Salaam, ambao ndiyo mabingwa watetezi, Vipers ya Uganda, JKU ya Zanzibar na Kator FC ya Sudan Kusini.

    Singida United imepewa nafasi ya Yanga SC kwenye michuano ya Kagame Cup 

    Kundi B litakuwa na timu za  Rayon Sport ya Rwamda, Gor Mahia ya Kenya, Lydia Ludic ya Burundi na Ports ya Djibouti.
    Mechi za ufunguzi zitachezwa Ijumaa ya Juni 29,  kati ya JKU na Vipers Saa 8:00 mchana, Azam FC na Kator Saa 10:00 jioni na Singida United dhidi ya APR Saa 1:00 usiku Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam - wakati Jumamosi ya Julai 30 kutakuwa na mechi mbili, Ports ba Lydia Saa 8:00 mchana na Simba dhidi ya Dakadaha Saa 10:00 jioni Uwanja wa Taifa.
    Azam FC ndiyo mabingwa wa mwisho wa michuano hiyo ilipofanyika Tanzania, walipowafunga Gor Mahia 2-0 katika fainali Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam, mabao ya waliokuwa washambuliaji wake hatari, John Raphael Bocco dakika ya 17 na Muivory Coast, Kipre Herman Tchetche dakika ya 64.
    Na hiyo ndiyo ilikuwa michuano iliyomtoa mshambuliaji Mkenya, Michael Olunga ambaye kwa sasa anachezea Girona FC ya Hispania kwa mkopo kutoka Guizhou Zhicheng ya China.
    Baada ya kufungha mabao matano akiwa na Gor Mahia na kuibuka mfungaji bora akiwapiku , Osman Bilal Salaheldin wa Al-Khartoum ya Sudan aliyefunga mabao manne sawa na Tchetche wa Azam FC, Olunga akachukuliwa na Djurgardens IF ya Sweden mwaka 2016 iliyomuuza Guizhou Zhicheng mwaka 2017.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SINGIDA UNITED WACHUKUA NAFASI YA YANGA KOMBE LA KAGAME, SIMBA KUFUNGUA DIMBA NA WASOMALI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top