• HABARI MPYA

    Monday, November 06, 2017

    SIMBA WAENDA ‘KUWAPA RAHA’ MASHABIKI WAO KATAVI

    Na David Nyembe, MBEYA 
    KIKOSI cha Simba kimeondoka leo asubuhi mjini Mbeya kwenda Katavi kwa ajili ya mchezo wa kirafiki dhidi ya wenyeji wao.
    Mratibu wa Simba SC, Abbas Suleiman ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online leo kwamba wanakwenda Katavi kwa mchezo mmoja wa kirafiki utakaochezwa kesho na Jumatano watarejea Mbeya.
    Simba SC ambayo jana ilirudi kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya Mbeya City Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, itakuwa na mchezo mwingine wa Ligi Kuu mkoani hapa dhidi ya Tanzania Prisons Novemba 18. 
    Simba SC jana imerudi kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya Mbeya City 

    Mchezo huo uko mbali kwa sababu umepisha kalenda ya mechi za Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), zikiwemo za kirafiki na kufuzu Kombe la Dunia. Wachezaji kadhaa wa Simba wanatarajiwa kuondoka kwenda kujiunga na timu zao za taifa na watakaobaki ndio watakwenda Katavi. 
    Na Abbas amesema baada ya mchezo wa kesho kikosi kitarejea Mbeya kuendelea na kambi ya maandalizi, ila ukitokea mchezo mwingine wa kirafiki na benchi la Ufundi likauafiki watakwenda kucheza. 
    Katika mchezo wa jana uliochezeshwa na refa Ahmed Kikumbo aliyesaidiwa na Omari Juma wote wa Dodoma na Michael Mkongwa kutoka Njombe, Simba ilipata bao hilo kipindi cha kwanza, likifungwa na winga, Shiza Ramadhani Kichuya. 
    Kichuya alifunga bao hilo dakika ya saba baada ya mabeki wa Mbeya City kusita kumdhibiti wakidhani ameotea kufuatia pasi ndefu ya juu ya kiungo Jonas Mkude. 
    Ushindi huo unaifanya Simba ifikishe pointi 19 baada ya kucheza mechi tisa na kupanda kileleni ikiizidi kwa wastani wa mabao tu Azam yenye pointi 19 pia. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA WAENDA ‘KUWAPA RAHA’ MASHABIKI WAO KATAVI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top