• HABARI MPYA

    Thursday, April 11, 2024

    BARCELONA YAWACHAPA PSG 3-2 PALE PALE PARIS


    WENYEJI, Paris Saint-Germain wamechapwa mabao 3-2 na Barcelona katika mchezo wa kwanza  wa Robó Fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya usiku huu Uwanja wa Parc des Princes Jijini Paris nchini Ufaransa.
    Mabao ya Barcelona yamefungwa na  mshambuliaji Mbrazil, Raphael Dias Belloli ‘Raphinha’ dakika ya 37 na 62 na beki Mdenmark, Andreas Bødtker Christensen dakika ya 77, wakati ya PSG yamefungwa na mshambuliaji Mfaransa, Masour Ousmane Dembélé dakika ya 48 na kiungo Mreno, Vítor Machado Ferreira ‘Vitinha’ dakika ya 50.
    Timu hizo zitarudiana Aprili 16 Uwanja wa Olímpic Lluís Companys Jijini Barcelona nchini Hispania na mshindi wa jumla atakutana na mshindi wa jumla ya kati ya Atletico Madrid ya Hispania na Borussia Dortmund ya Ujerumani.
    Atletico Madrid imejiweka kwenye nafasi nzuri ya kwenda Nusu Fainali baada ya ushindi wa 2-1 dhidi ya Borussia Dortmund Uwanja wa Cívitas Metropolitano Jijini Madrid.
    Mabao ya Atletico Madrid yamefungwa na Rodrigo Javier De Paul dakika ya nne na Samuel Lino dakika ya 32, wakati bao pekee la Borussia Dortmund  limefungwa na Sébastien Haller dakika ya 81.
    Timu hizo zitarudiana Aprili 16 Uwanja wa Signal Iduna Park Jijini Dortmund.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BARCELONA YAWACHAPA PSG 3-2 PALE PALE PARIS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top