• HABARI MPYA

    Sunday, November 12, 2023

    JKT QUEENS YAFUNGISHWA VIRAGO LIGI YA MABINGWA AFRIKA WANAWAKE


    TIMU ya JKT Queens jana wametupwa nje ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa wanawake baada ya kuchapwa mabao 4-1 na AS Casablanca ya Morocco katika mchezo wake wa mwisho wa Kundi A jana Uwanja wa Laurent Pokou mjini San-Pedro nchini Ivory Coast.
    Mabao ya AS Casablanca yalifungwa na kiungo Meryem Hajri kwa penalti dakika ya 30, mshambuliaji Chaymaa Mourtaji dakika ya 39, na wa wanasoka wa Kimataifa wa Ivory Coast, kiungo N'Guessan Nadège Koffi dakika ya 42 na mshambuliaj Sylviane Kokora Adjoua dakika ya 58, huku bao pekee la JKT Queens likifungwa na mshambuliaji Stumai Abdallah Athumani dakika ya 56.
    JKT Queens, mabingwa wa Tanzania na Afrika Mashariki na Kati, 
    walimaliza pungufu mchezo huo baada ya wachezaji wake wawili kutolewa kwa kadi nyekundu, Happyness Hezron Mwaipaja dakika ya 29 na Anastazia  Nyandago Simba dakika ya 85.
    Queens iliingia kwenye mchezo huo bila nyota wake sita ambao kwa pamoja na Mshauri Mkuu wa Ufundi w timu, Bakari Nyundo Shime walilazimika kurejea nyumbani kujunga na timu ya taifa ya wasichana chini ya umri wa miaka 20 kwa ajili ya mchezo wa Kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Nigeria leo Jijini Dar es Salaam.
    Kwa matoke ohayo, Queens inamaliza nafasi ya tatu kwenye kundi lake ikiwa na pointi tatu, mbele ya wenyeji, Athlético Abidjan waliovuna pointi moja tu – huku Mamelodi Sundowns iliyomaliza kwa ushindi wa 3-0 dhidi ya Athlético Abidjan Uwanja wa Amadou Gon Coulibaly mjini Korhogo nchini hapa na kuongoza kwa pointi zake tisa na AS Casablanca yenye pointi nne zikienda Nusu Fainali.
    Mechi za mwisho za Kundi B zinachezwa leo Saa5:00 usiku, Mandé ya Mali na mabingwa watetezi, FAR Rabat Uwanja wa Laurent Pokou na Ampem Darkoa ya Ghana dhidi ya Huracanes ya Equatorial Guinea Uwanja wa Amadou Gon Coulibaly.
    Kwa sasa ni Mandé ndio inaongoza Kundi B kwa pointi zake nne, ikifuatiwa Ampem Darkoa yenye pointi tatu sawa na mabingwa watetezi, FAR Rabat wakati Huracanes yenye pointi moja inashika mkia.
    Ikumbukwe Bingwa wa michuano hii anapata dola za Kimarekani 400,000, mshindi wa pili 250,000, waliokwenda Nusu Fainali 200,000, wanaomaliza nafasi ya tatu kwenye Kundi 150,000 na wanaoshika mkia dola 100,000.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: JKT QUEENS YAFUNGISHWA VIRAGO LIGI YA MABINGWA AFRIKA WANAWAKE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top