• HABARI MPYA

    Thursday, November 16, 2023

    KINDA WA AZAM FC KACHWELE AJIUNGA NA VANCOUVER WHITECAPS


    CHIPUKIZI wa Azam FC, Cyprian Kachwele amejiunga na klabu ya Vancouver Whitecaps ya Cañada inayoshiriki Ligi Kuu ya Marekani (MLS).
    Azam FC imetoa taarifa rasmi ya kumuaga na kumtakia kila la heri katika maisha mapya Vancouver Whitecaps inayofundishwa na Kocha Mtaliano, Vanni Sartini.
    “Tunamtakia kila la kheri mshambuliaji wetu chipukizi, Cyprian Kachwele, aliyejiunga na timu yake mpya ya Vancouver Whitecaps inayoshiriki Ligi Kuu ya Marekani (MLS),” imesema Taarifa ya Azam FC.
    Kachwele aliibukia akademi ya Azam FC, kabla ya kupandishwa timu kubwa mwishoni mwa msimu uliopita na kucheza baadhi ya mechi, akifunga mabao matatu katika mechi za mashindano.
    Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 18, anakuwa Mtanzania wa tatu Kihistoria kusajiliwa 
    Vancouver Whitecaps baada ya beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ aliyechukuliwa kwa mkopo katí ya 2009 na 2010 na kiungo Nizar Khalfan kuanzia 2009 hadi 2011.
    Nizar alifanikiwa kuwa mchezaji tegemeo Vancouver Whitecaps na kucheza jumla ya mechi 48 katika msimu hiyo miwili akifunga mabao matatu na kutoa pasi za mabao 23,
    kabla ya kurejea nyumbani kumalizia soka yake ya Yanga na sasa ni Kocha Msaidizi wa Singida Fountain Gate.
    Mambo hayakuwa mazuri kwa Cannavaro ambaye hakucheza mechi yoyote ya mashindano na mwisho wa mkopo wake akarejea Jangwani ambako alicheza hadi kustaafu mwaka 2018.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KINDA WA AZAM FC KACHWELE AJIUNGA NA VANCOUVER WHITECAPS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top