• HABARI MPYA

    Wednesday, July 25, 2018

    MASHINDANO YA VIJANA U-15, U-17, U-20 KUANZA OKTOBA HADI APRILI 2019

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MASHINDANO ya vijana nchini yanatarajiwa kufanyika kati ya Mwezi Oktoba 2018 na April 2019 kama ambavyo Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wallace Karia alitangaza msimu huu kutawepo Mashindano ya Vijana kwa wachezaji wenye umri chini ya miaka 15,17 na 20.
    Katika marekebisho ya Kanuni msimu wa 2018-2019 vilabu vyote vya Ligi Kuu, Ligi Daraja la Kwanza na Ligi Daraa la Pili vinalazimika kuwa na timu za Vijana.
    Timu za Ligi Kuu zinapaswa kuwa na timu za vijana chini ya miaka 20 (U-20) na chini ya miaka 17 (U-17), huku timu za Daraja la Kwanza na Daraja la Pili zikitakiwa kuwa na timu za vijana wenye umri chini ya miaka 17 (U-17).

    Ligi ya U20 itaanza Oktoba ikishirika timu za vijana (U-20) kwa vilabu vyote kwa mtindo wa nyumbani na ugenini, huku Mashindano ya U17 yatakyoshirikisha timu 68 za vijana kutoka vilabu vya Ligi Kuu, Daraja la Kwanza na Daraja la Pili yakitarajiwa kuanza Novemba, 2018.
    Michuano ya U15 itashirikisha jumla ya timu 35 kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani ambayo inatarajiwa kuchezwa mwezi Desemba, 2018.
    Katika hatua nyingine, pazia la usajili kwa wachezaji wa timu za vijana chini ya umri wa miaka 20 (U20) na miaka 17 (U17) litafungwa Agosti 17, mwaka huu.
    Taarifa ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imesema kwamba kila klabu inaruhusiwa kusajili wachezaji wasiozidi 22 kwa timu ya U-20 na wachezaji wasiozidi 22 kwa timu ya U-17.
    TFF imesema nyaraka za kuambatanishwa kwenye mfumo wa usajili ni Cheti cha Kuzaliwa au Kitambulisho cha Uraia na Pasipoti ya kusafiria, Fomu ya kumaliza Shule ya Msingi (TSM9), Cheti Cha Daktari, Mkataba (makubaliano), Historia ya mchezaji (Players Passport), Majina matatu yaliyopo kwenye kitambulisho/cheti na picha (passport size).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MASHINDANO YA VIJANA U-15, U-17, U-20 KUANZA OKTOBA HADI APRILI 2019 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top