• HABARI MPYA

    Tuesday, July 24, 2018

    HASSAN KABUNDA AJIUNGA NA KMC KAMA MCHEZAJI HURU KUTOKA MWADUI FC

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni (KMC) imeendelea kuimarisha kikosi chake kuelekea msimu ujao wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya leo kumsainisha mkataba wa mwaka mmoja, kiungo mshambuliaji, Hassan Salum Kabunda kutoka Mwadui FC.
    Meneja wa KMC, Walter Harrison ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online leo kwamba Kabunda amejiunga na KMC kama mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake Mwadui FC.
    Mtoto huyo wa beki wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Salum Kabunda ‘Ninja’ (sasa marehemu) aliyewika Yanga SC aliibukia katika kituo cha kukuza vipaji Dar es Salaam (DYOC) kabla ya kuchezea timu ya vijana ya Ashanti United, ambako alipandishwa hadi timu ya wakubwa na kuanzia huko kucheza Ligi Kuu.

    Meneja wa KMC, Walter Harrison (kulia) akimkabidhi mkataba Hassan Kabunda (katikati) leo mjini Dar es Salaam

    Baada ya Ashanti kuremka daraja, Kabunda ambaye mchezo wake wa kwanza Ligi Kuu ulikuwa dhidi ya JKT Ruvu, sasa JKT Tanzania akifunga bao zuri lililompatia umaarufu, alienda kujiunga na Mwadui ambayo anaachana nayo sasa kurejea Dar es Salaam.
    Kabunda anakuwa mchezaji mpya wa tano kusajiliwa KMC baada ya kipa Juma Kaseja kutoka Kagera Sugar na mabeki Aaron Lulambo, Ali Ali wote kutoka Stand United, Sadallah Lipangile kutoka Mbao FC na kiungo mshambuliaji, Abdul Hillary Hassan kutoka Tusker FC ya Kenya.
    Kwa upande wa wachezaji waliopandisha timu hiyo Ligi Kuu chini ya Freddy Felix Minziro waliopewa mikataba mipya hadi sasa ni sita tu, ambao ni beki wa pembeni Ally Ramadhani, viungo Cliff Buyoya, Abdulhalim Humud na Adam Kingwande, Rayman Mgungila na mshambuliaji Rehan Kibingu.
    Tayari Minziro amekwishaondolewa na nafasi yake imechukuliwa na Mrundi Ettienne Ndayiragijje ambaye misimu miwili iliyopita alikuwa Mbao FC ya Mwanza.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HASSAN KABUNDA AJIUNGA NA KMC KAMA MCHEZAJI HURU KUTOKA MWADUI FC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top