• HABARI MPYA

    Friday, July 27, 2018

    CANNAVARO APEWA UMENEJA YANGA, MZIMBABWE WA SINGIDA UNITED APIGWA CHINI

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    NAHODHA wa muda mrefu wa Yanga SC, Nadir Haroub Ali ‘Cannavaro’ amestaafu soka na kuteuliwa kuwa Meneja wa timu akichukua nafasi ya Hafidh Saleh ambaye sasa anakuwa Mratibu wa timu.
    Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Hussein Nyika ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online leo kwamba baada ya mchango wa muda mrefu kama mchezaji, Cannavaro sasa anahamia kwenye benchi la Ufundi.
    Cannavaro alijiunga na Yanga mwaka 2006 kutoka Malindi FC ya kwao, Zanzibar na mwaka 2009 alitolewa kwa mkopo wa miezi sita kwenda klabu ya Vancouver Whitecaps ya Canada iliyokuwa inashiriki Ligi ya Marekani, kabla kurejea kucheza timu ya Jangwani hadi msimu uliopita.
    Nadir Haroub ‘Cannavaro’ sasa anakuwa Meneja wa Yanga baada ya kustaafu soka kufuatia kuichezea tangu mwaka 2006 

    Nadir Haroub 'Cannavaro' katika msimu wake wa kwanza Yanga SC mwaka 2006 wakisalimiana na Miss Tanzania, Nancy Sumary

     imesajili wachezaji 28 wa kikosi cha kwanza kuelekea msimu ujao ni pamoja na makipa watatu, Benno Kakolanya, Klaus Kindoki kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Mcameroon, Youthe Rostand; mabeki ni Juma Abdul, Cleophas Sospter, Mwinyi Mngwali, Gardiel Michael, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na Andrew Vincent ‘Dante’.
    Viungo ni Mkongo Pius Buswita, Mohammed Issa 'Banka', Papy Kabamba Tshishimbi, Mzimbabwe Thabani Kamusoko, Jafar Mohammed, Raphael Daudi, Said Juma ‘Makapu’, Feisal Salum, Deus Kaseke, Emmanuel Martin, Juma Mahadhi, Pato Ngonyani na Paulo Godfrey.
    Washambuliaji ni Matheo Anthony, Mrisho Ngassa, Amissi Tambwe, Ibrahim Ajib, Haritier Makambo, Yussuh Mhilu na Yahya Akilimali. Aidha, kikosi hicho cha kwanza kitakuwa kinaongezewa nguvu na wachezaji wanne wa timu vijana, ambao ni kipa Ramadhan Kabwili, viungo Maka Edward, Said Mussa na mshambuliaji Yohanna Nkomola.
    Pamoja na hayo, Nyika amesema wameachana na beki Mzimbabwe, Elisha Muroiwa kutoka Singida United baada ya mapendekezo ya kocha wao, MMwinyi Zahera.
    Yanga SC inatarajiwa kuteremka uwanjani Jumapili, kumenyana na Gor Mahia FC ya Kenya katika mchezo wa Kundi D Kombe la Shirikisho Afrika kuanzia Saa 1:00 usiku Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Mechi hiyo itachezeshwa na marefa kutoka Mauritius ambao ni Ahmad Imtehaz Heeralall atakayepuliza filimbi akisaidiwa na Cauvelet Louis Ralph Fabien na Akhtar Nawaz Rossaye washika vibendera. 
    Yanga haijashinda mechi hata moja kati ya tatu za awali, ikifungwa mbili zote 4-0, ya kwanza dhidi ya MC Alger nchini Algeria Mei 6 na ya pili dhidi ya Gor Mahia Julai 18 mjini Nairobi wakati nyingine walitoka sare ya 0-0 na Rayon Sport mjini Dar es Salaam Mei 16. 
    Baada ya mechi na Gor Jumapili, Yanga wataikaribisha USM Alger Agosti 19 kabla ya kwenda kukamilisha mechi zake za kundi hilo kwa kumenyana na wenyeji, Rayon Sport Agosti 28.
    Habari njema kuelekea mchezo huo ni wachezaji wawili, kiungo Deus Kaseke na mshambuliaji Matheo Anthony kupatiwa leseni na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kucheza mechi hizo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: CANNAVARO APEWA UMENEJA YANGA, MZIMBABWE WA SINGIDA UNITED APIGWA CHINI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top