• HABARI MPYA

    Sunday, March 26, 2017

    SERENGETI BOYS WAKO BUKOBA, IKIRUDI KUIVAA GHANA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya taifa ya soka vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys itamenyana na Ghana Aprili 5, mwaka katika mchezo wa kirafiki Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alfred Lucas amesema leo kwamba, mchezo huo utakuwa maalum kuwaaga mashabiki kabla ya kwenda Morocco kwenye kambi ya mwisho ya kujiandaa na fainali za U-17 Afrika Mei mwaka huu nchini Gabon.
    Serengeti leo imewasili Bukoba mkoani Kagera leo kwa ndege ya Shirika la Tanzania (ATCL) kutoka Dar es Salaam kwa kambi ya wiki moja. 
    Serengeti Boys itakuwa kambini Bukoba hadi Aprili 2, mwaka huu ambako inatarajiwa kucheza michezo miwili ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya timu vijana ya Burundi kwenye Uwanja wa Kaitaba, mjini Bukoba mkoani Kagera. 
    Michezo hiyo itafanyika Machi 30, 2017 na kurudiana Aprili mosi, mwaka huu. 
    Serengeti Boys itarejea Dar es Salaam Aprili 2 kucheza na Ghana Aprili 3, mchezo ambao utatanguliwa na hafla ya kuagwa kwa kukabidhiwa bendera na Waziri wa Michezo, Dk Harison Mwakyembe.
    Wachezaji wa Serengeti Boys wamewasili Bukoba leo kwa kambi ya wiki moja kabla ya kwenda Morocco

    Timu itaelekea Morocco Mei 5, mwaka huu baadaye itapita Cameroon kwenye kambi ya zaidi ya mwezi mmoja baadaye itakwenda Gabon katika michuano itakayoanza Mei 14, 2017. 
    Ikiwa Cameroon itacheza mechi mbili za kimataifa dhidi ya wenyeji kabla ya kwenda kwenye fainali. 
    Serengeti Boys ni timu ya vijana ambayo imefuzu kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazofanyika Gabon kuanzia Mei 14, mwaka huu. Timu hiyo imepangwa Kundi ‘B’ pamoja na mabingwa watetezi Mali, Niger na Angola. Ina lengo la kurejea na Kombe la Afrika kwa vijana. 
    La ikitokea imekosa nafasi hiyo angalau ikafika nusu fainali ambako kwa mafanikio hayo itakuwa tayari ina tiketi mkononi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia huko India, Novemba, mwaka huu. 
    Kikosi cha Serengeti Boys kinaundwa na Makipa:  Ramadhan Kabwili, Samwel Edward na Kelvin Kayego. 
    Walinzi: Kibwana Ally Shomari, Nickson Kibabage, Israel Mwenda, Dickson Job, Ally Msengi, Issa Makamba na Enrick Vitalis Nkosi. 
    Viungo: Kelvin Nashon Naftali, Ally Ng’anzi, Mohamed Rashid, Shaaban Ada, Mathias Juan, Marco Gerald, Abdulhamis Suleiman, Saidi Mussa na Cyprian Benedictor Mtesigwa.
    Washambuliaji:  Muhsin Malima Makame, Yohana Mkomola, Ibrahim Abdallah, Assad Juma na Abdul Suleiman.
    Benchi la Ufundi linaundwa na Bakari Shime (Kocha Mkuu), Oscar Mirambo (Kocha Msaidizi), Muharami Mohamed (Kocha wa makipa), Kim Poulsen (Mshauri wa Ufundi), Edward Evans (Mtunza Vifaa) na Shecky Mngazija (Daktari wa timu).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERENGETI BOYS WAKO BUKOBA, IKIRUDI KUIVAA GHANA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top