• HABARI MPYA

    Saturday, March 25, 2017

    SAMATTA AFUNGA YOTE MAWILI, TAIFA STARS YAIPIGA 2-0 BOTSWANA

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    MABAO mawili ya Nahodha Mbwana Ally Samatta yametosha kuipa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Botswana katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Huo ulikuwa mchezo wa kwanza Taifa Stars inacheza chini ya kocha wake mpya, Salum Mayanga aliyerithi mikoba ya Charles Boniface Mkwasa aliyeng’atuka Janauri.
    Katika mchezo huo uliodhuhuriwa na Waziri mpya wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, DK Harison Mwakyembe, ilimchukua dakika mbili tu mshambuliaji huyo wa KRC Genk ya Ubelgiji kuwainua vitini wapenzi wa soka wa Tanzania waliojitokeza Uwanja wa Taifa baada ta kupokea pasi ya winga Shiza Kichuya na kumtoka beki Kaone Vanderwesthuizem kabla ya kumchambua kipa, Kabelo Dambe.
    Nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta akikimbia kushangilia baada ya kufungaa bao la kwanza leo
    Samatta akimtoka beki wa Botswana kabla ya kufunga bao la kwanza
    Simon Msuva akimiliki mpira mbele ya wachezaji wa Botswana
    Mshambuliaji Ibrahim Hajib wa Tanzania akimtoka beki wa Botswana
    Beki wa Tanzania, Shomary Kapombe akiambaa na mpira pembezoni mwa Uwanja

    Baada ya bao hilo, Botswana wakabadilisha aina ya uchezaji na kuacha kujilinda zaidi na badala yake kuanza kupeleka mashambulizi langoni mwa Stars.
    Hali hiyo iliitia misukosuko kidogo ngome ya Taifa Stars, lakini siofa zimuendee kipa Aishi Salum Manula aliyeokoa hatari zote. 
    Kipindi cha pili, mchezo uliendelea kuwa wa kushambuliana kwa zamu, ingawa Stars ndiyo wal8oendelea kung’ara zaidi uwanjani.
    Wafungaji hodari katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Shiza Kichuya wa Simba SC na Simon Msuva wa Yanga haikuwa bahati yao leo, kwani walipoteza nafasi kadhaa nzuri za kufunga.
    Winga Farid Mussa wa Tenerife ya Hispania alimkatia pasi nzuri Nahodha Samatta na wakati analielekea lango la Botswana akaangushwa na Thero Setsile nje kidogo ya boksi.
    Samatta akaenda mwenyewe kupiga shuti la mpira wa adhabu kiufundi na kuifungia bao la pili Taifa Stars dakika ya 87.
    Kikosi cha Tanzania kilikuwa: Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Erasto Nyoni, Abdi Banda, Himid Mao/Jonas Mkude, Simon Msuva/Said Ndemla, Frank Domayo/Muzamil Yassin, Mbwana Samatta, Ibrahim Hajib na Shiza Kichuya/Farid Mussa. 
    Botswana: Kabelo Dambe, Tapiwa Gadibolae, Kaone Vanderwesthuizem, Lesenya  Ramoraka, Lesego Galenamotlhale, Ofentse Nato, Lebogang Ditsele, Omaaatla Kebatho, Mosha Gaolaolwe, Thacng Sesenyi na Mogakolod Ngele.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA AFUNGA YOTE MAWILI, TAIFA STARS YAIPIGA 2-0 BOTSWANA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top