• HABARI MPYA

    Tuesday, January 12, 2016

    SAMATTA ‘MGENI WA HESHIMA’ FAINALI KOMBE LA MAPINDUZI ZANZIBAR KESHO

    Na Mwandishi Wetu, ZANZIBAR
    MWANASOKA Bora Anayecheza Afrika, Mbwana Ally Samatta kesho atatambulishwa kwa Wazanzibari wakati wa mchezo wa fainali ya Kombe la Mapinduzi, kati ya Mtibwa Sugar na URA ya Uganda.
    Katibu wa Kamati ya Kombe la Mapinduzi, Mwinyimvua Khamis ameiambia BIN ZUBEIRY SPORTS – ONLINE leo kwamba Samatta atawasili kesho Uwanja wa Amaan na kusalimia mashabiki pamoja na kuinua tuzo yake kuinoyesha.
    Samatta, mshambuliaji wa kimataifa wa Tanzania na klabu bingwa Afrika, TP Mazembe ya DRC, anatarajiwa kuketi pamoja na viongozi wakuu wa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kesho wakati mchezo huo ukiendelea.
    Wazanzibari watapata fursa ya kusherehekea na Samatta kesho Uwanja wa Amaan
     

    Ikumbukwe ni jana tu Samatta amepatiwa viza ya kwenda Ubelgiji kujiunga na klabu ya KRC Genk ya Ligi Kuu ya nchini humo.
    Ingawa bado klabu yake, TP Mazembe haijatangaza rasmi, lakini taarifa zinasema mwishoni mwa mwaka jana, Rais wa klabu hiyo ya DRC, Moise Katumbi alifikia makubaliano na klabu hiyo ya Ubelgiji juu ya biashara ya mchezaji huyo.
    Na kwa Samatta kwa kupatiwa viza ya kwenda Ubelgiji, maana yake anahitimisha miaka yake minne ya kuishi Lubumbashi, yalipo makao makuu ya TPM, klabu bingwa ya Afrika mara ya tano.
    Samatta aliyejiunga na TPM mwaka 2011 akitokea Simba SC aliyoichezea kwa nusu msimu, akitokea African Lyon, anaondoka Mazembe baada ya kuichezea mechi 103 na kuifungia mabao 60.
    Kijana huyo wa umri wa miaka 24, anaondoka Mazembe akiiachia taji la Ligi ya Mabingwa Afrika, huku naye akiibuka mfungaji bora wa michuano hiyo na kutwaa tuzo ya Mchezaji Bora Anayecheza Afrika.   
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA ‘MGENI WA HESHIMA’ FAINALI KOMBE LA MAPINDUZI ZANZIBAR KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top