• HABARI MPYA

    Saturday, January 30, 2016

    TEMBO WA IVORY COAST WAUA SIMBA WA CAMEROON 3-0 NA KUTINGA NUSU FAINALI

    TEMBO wa Ivory Coast wameua Simba Wasiofungika wa Cameroon na kutinga Nusu Fainali ya Michuano ya Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN) mjini Kigali, Rwanda leo.
    Dakika 90 zilimalizika timu hizo zikiwa hazijafungana na katika dakika 30 za nyongeza ndipo Cameroon wakatepeta na kuruhusu mabao matatu.
    Koffi Boua alifunga bao la kwanza dakika ya 95 kwa pasi ya Serge N’Guessan, kabla ya Djobo Atcho kufunga la pili dakika ya 102 kwa pasi ya 
    Krahire Zakri na N’Guessan akafunga la tatu dakika ya 112 kwa pasi ya Cheick Comara.

    Mapema katika mchezo uliotangulia, wenyeji Rwanda walitupwa nje na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kwa kufungwa 2-1  katika mchezo uliodumu kwa dakika 120 pia, baada ya dakika 90 kumalizika sare ya 1-1.
    Hatimaye Botuli Padou Bompunga akaibuka shujaa wa DRC kwa kufunga bao la ushindi dakika ya 114 na ‘kuwaliza’ maelfu ya Wanyarwanda waliojitokeza kwa wingi Uwanja wa Amahoro kuishangilia Amavubi.
    DRC walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Doxa Gikanji dakika ya 11, kabla ya Ernest Sugira kuisawazishia Rwanda dakika ya 56 akimalizia pasi ya Jean Claude Iranzi.
    Robo Fainali za mwisho za michuano hiyo inayoshirikisha wachezaji wanaocheza ligi za nchini mwao pekee, zitachezwa kesho, kati ya 
    Tunisia na Mali na Zambia na Guinea.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TEMBO WA IVORY COAST WAUA SIMBA WA CAMEROON 3-0 NA KUTINGA NUSU FAINALI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top