• HABARI MPYA

    Wednesday, July 24, 2013

    AZAM FC YATAKIWA KUBOMOA BENKI KUSAJILI MSHAMBULIAJI WA NGUVU

    Na Mahmoud Zubeiry, IMEWEKWA JULAI 24, 3013 SAA 2: 39 ASUBUHI
    AZAM FC italazimika kubomoa benki na kusajili japokuwa mshambujliaji mmoja wa nguvu, kufuatia kuumia kwa wachezaji wake wawili wa kigeni, kiungo mshambuliaji, Mkenya Humphrey Mieno na mshambuliaji Mganda, Brian Umony.
    Wachezaji wote hao wanatakiwa kuwa nje kwa mwezi mmoja, lakini kulingana na maumivu yao, wanaweza kuchukua muda zaidi ya huo.
    Pacha wakali; Mfungaji bora Ligi Kuu, Kipre Tchetche akiwa ameshika na mdogo wake, Kipre Balou tuzo ya ufungaji bora. Wote wawili ni wachezaji wa kikosi cha kwanza Azam FC.

    Kutokana na ukweli kwamba hata mshambuliaji mzawa John Bocco ‘Adebayor’ msimu uliopita aliandamwa na majeruhi- Azam italazimika kusajili mshambuliaji wa nguvu kama kweli inataka kushindana na Simba na Yanga katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu.
    Majeruhi; Mganda Brian Umony ameumia na anatakiwa kuwa nje kwa zaidi ya mwezi mzima, jambo ambalo litawalazimu Azam kusajili mchezaji mwingine wa kuziba pengo lake

    Kocha Muingereza, Stewart Hall alisema hahitaji kusajili wakati huu na atasubiri hadi Januari wakati wa dirisha dogo kwa kuwa atakuwa anafanya usajili mkubwa wa hadi michuano ya Afrika- lakini wakati huo matatizo ya Mieno na Umony yalikuwa hayajajitokeza. 
    Mshambuliaji mkongwe, Gaudence Mwaikimba pamoja na kukubalika mbele ya Stewart, lakini haaminiwi sana na Muingereza huyo, ingawa akipewa nafasi anafanya kazi nzuri.
    Seif Abdallah Karihe aliyesajiliwa Januari kutoka Ruvu Shooting bado hajaaminiwa sana na Stewart, ingawa naye pia akipewa nafasi huwa anafanya vitu.
    Mshambuliaji pekee anayekubaliwa na kuaminiwa na Stewart kwenye kikosi cha Azam ukiondoa John Bocco ni Kipre Tchetche raia wa ivory Coast. Tchetche alirithi kiatu cha dhababu cha ufungaji bora wa Ligi Kuu msimu uliopita kutoka kwa Bocco.
    Haaminiki; Mwaikimba huwa anafunga akipewa nafasi, lakini bado Stewart hamuamini sana

    Katika safu ya kiungo, japokuwa Abdulhalim Humud na Abdi Kassm ‘Babbi’ wameondolewa, lakini hakuna tatizo kwa kuwa wapo Salum Abubakar ‘Sure Boy’, Kipre Balou, Ibrahim Mwaipopo na Jabir Aziz, Khamis Mcha 'Vialli' pamoja na Himid Mao, ambaye kwa sasa anachezeshwa beki ya kulia. Kiungo wa timu ya vijana, Mudathir Yahya anapandishwa kuongeza idadi ya watu katika eneo hilo.
    Ukuta wa Azam nao uko vizuri- mabeki wa kati ni Joackins Atudo, David Mwantika, Said Mourad, Aggrey Morris na Luckson Kakolaki.
    Pembeni, kulia Himid anacheza na bado kuna Erasto Nyoni, wakati kushoto wapo Waziri Salum, Malika Ndeule na Samih Hajji Nuhu. Timu itakuwa na makipa wawili wa timu ya taifa, Mwadini Ally na Ashi Manula.
    Hakuwa asilimia mia; Msimu uliopita John Bocco hakuwa fiti kwa asilimia 100 ndiyo maana akasajiliwa Umony

    Ligi Kuu inatarajiwa kuanza Agosti 24, mwaka huu wakati Azam FC itapambana na Yanga SC, wiki moja kabla (Agosti 17) kuwania Ngao ya Jamii, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 
    Msimu huu Ligi Kuu inatarajiwa kuwa ngumu na ushindani utakuwa mkubwa kutokana na harufu ya kupatikana kwa mdhamini mpya, Azam TV ambaye atagawa si chini ya Sh. Milioni 100 kwa kila timu.
    Dhahiri Azam wanahitaji kujipanga sawa sawa kama kweli wanataka kutimiza ndoto za kutwaa taji la kwanza la Ligi Kuu msimu huu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: AZAM FC YATAKIWA KUBOMOA BENKI KUSAJILI MSHAMBULIAJI WA NGUVU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top