• HABARI MPYA

    Sunday, July 15, 2018

    UFARANSA BINGWA WA DUNIA 2018, LUKA MODRIC MCHEZAJI BORA

    Na Mwandishi Wetu, MOSCOW
    TIMU ya taifa ya Ufaransa imetwaa ubingwa wa dunia kwa mara ya kwanza tangu 1998 baada ya ushindi wa mabao 4-2 dhidi ya Croatia katika mchezo mzuri wa fainali uliofanyika Uwanja wa Luzhniki mjini Moscow, Urusi.
    Ahsante kwa wafungaji wa mabao ya Ufaransa leo, Antoine Griezmann, Paul Pogba, Kylian Mbappe na Mario Mandzukic aliyejifunga na kikosi cha kocha Didier Deschamps sasa kinasherehekea Kombe la Dunia.
    Ufaransa ilipata bao lake la kwanza dakika ya 18 baada ya Mario Mandzukic kujifunga kufuatia mpira wa adhabu, kabla ya Croatia kusawazisha dakika ya 28 kupitia kwa Ivan Perisic.
    Wachezaji wa Ufaransa wakishangilia ubingwa wa dunia baada ya ushindi wao wa 4-2 dhidi ya Croatia 

    Ufaransa wakazawadiwa penalti dakika ya 36 baada ya Teknlojia ya Msaada wa Video (VAR) kuthibitisha Perisic aliunawa mpira na Antoine Griezmann akaenda kufunga kwa shuti zuri.
    Kiungo wa Manchester United, Paul Pogba akaupendezesha ushindi wa Ufaransa kwa bao la tatu dakika ya 59 alipofumua shuti kali kabla ya Kylian Mbappe kufunga la nne dakika sita baadaye.
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Nestor Pitana kutoka Argentina, Mandzukic akaifungia bao la pili la kufutia machozi Croatia dakika ya 69 akitumia makosa ya kipa wa Ufaransa, Hugo Lloris.
    Mshambulijai wa England iliyomaliza nafasi ya nne baada ya kufungwa 2-0 na Ubelgiji jana, Harry Kane amekuwa mfungaji bora kwa mabao yake sita akifuatiwa na Romelu Lukaku wa Ubelgiji na Antoine Griezmann wa Ufaransa waliomaliza na mabao manne.
    Luka Modric amekuwa Mchezaji Bora wa mashindano hayo, huku Mbappe akitwaa Tuzo ya Mchezaji Bora Chipukizi wa Mashindano na Griezmann amekuwa Mchezaji Bora wa Mechi.
    Mlinda mlango wa Ubelgiji, Thibaut Courtois amekuwa Kipa Bora wa Mashindano wakati Hispania imetwa tuzo ya Soka ya Kiungwana.  
    Kikosi cha Ufransa kilikuwa: Lloris, Pavard, Varane, Umtiti, Hernandez, Pogba, Kante/N’Zonzi dk55, Mbappe, Griezmann, Matuidi/Tolisso dk73 na Giroud/Fekir dk81.
    Croatia; Subasic, Vrsaljko, Lovren, Vida, Strinic/Pjaca dk81, Rakitic, Brozovic, Rebic/Kramaric dk71, Modric, Perisic na Mandzukic.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: UFARANSA BINGWA WA DUNIA 2018, LUKA MODRIC MCHEZAJI BORA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top