• HABARI MPYA

    Tuesday, September 07, 2021

    TAIFA STARS YAICHAPA MADAGASCAR 3-2 DAR

     TIMU ya faifa ya Tanzania imeibuka na ushindi wa 3-2 dhidi ya Madagascar katika mchezo wa Kundi J kufuzu Kombe la Dunia uliofanyika Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Hadi mapumziko, timu hizo zilikuwa zimefungana 2-2, Taifa Stars ikitangulia kwa mabao ya kiungo wa Simba SC ya nyumbani, Erasto Edward Nyoni dakika ya kwanza tu kufuatia mshambuliaji wa Wydad Athletic ya Morocco, Simon Happygod Msuva kuangushwa kwenye boksi sekunde ya tano.
    Kiungo wa Maccabi Tel Aviv ya Israel, Novatus Dismas Miroshi akaifungia bao la pili Taifa Stars dakika ya 26 akimalizia kazi nzuri ya Nahodha na mshambuliaji wa Royal Antwerp ya au Ubelgiji, Mbwana Ally Samatta.


    Madagascar ikazinduka kwa mabao ya winga wa Suphanburi FC ya Thailand, Njiva Tsilavina Martin Rakotoharimalala dakika ya 36 na beki wa Lorient ya Ufaransa, Thomas Fontaine dakika ya 45 na ushei. 
    Na shujaa wa Taifa Stars leo amekuwa kiungo wa Yanga SC ya nyumbani, Feisal Salum Abdallah aliyefunga bao la ushindi dakika ya  52 akimalizia pasi ya Samatta.
    Kwa ushindi huo, Tanzania inapanda kileleni Kundi J ikifikisha pointi nne baada ya mechi mbili, kufuatia sare ya 1-1 na wenyeji, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) katika mchezo wa kwanza Alhamisi iliyopita.
    Benin inafuatia ikiwa na pointi nne pia, wakati DRC ni ya tatu kwa pointi zake mbili na Madagascar hawana pointi baada ya kufungwa nyumbani na ugenini mfululizo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TAIFA STARS YAICHAPA MADAGASCAR 3-2 DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top