MCHEZO namba 146
wa Ligi Kuu ya Vodacom baina
ya Mtibwa Sugar na Simba uliochezwa Machi 18 mwaka huu katika Uwanja wa Jamhuri,
Morogoro umeingiza sh. 31,230,000.
Ofisa habari wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF) Boniface
Wambura alisema jana kwamba fedha hizo zimepatikana kupitia watazamaji 10,410
waliokata tiketi kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 3,000.
“Baada ya kuondoa
gharama za awali za mchezo na asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT)
ambayo ni sh. 4,763,898.31 kila timu ilipata sh. 6,508,230.51, uwanja sh.
2,169,410.17,Chama cha soka Mkoa wa Morogoro (MRFA) sh. 867,764.07, TFF sh. 2,169,410.17, Mfuko wa Maendeleo wa soka
(FDF) sh. 1,084,705.08, Baraza la Michezo la Taifa (BMT) sh. 216,941.02 na
asilimia 10 ya gharama za mechi sh. 2,169,410.17”, Alisema Wambura.
Katika hatua nyingine timu za Villa Squad na JKT Ruvu leo
zitahitimisha raundi ya 21 ya ligi hiyo kupitia mchezo wao utakaopigwa kwenye
Uwanja wa Chamazi, jijini Dar es Salaam.
Aidha Machi 24 mwaka huu kutakuwa na mechi ya ligi hiyo kati
ya Moro United na African Lyon itakayopigwa pia kwenye dimba la Chamazi, kabla
ya Machi 28 mwaka huu Ruvu Shooting
Stars itakwaana na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mabatini mjini Mlandizi wakati
Moro United itakuwa mwenyeji wa Villa Squad itakayofanyika Uwanja wa Chamazi.
Wakati huo huo: Mkutano Mkuu wa kawaida wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF)
uliokuwa ufanyike Machi 24 na 25 mwaka huu jijini Dar es Salaam umesogezwa
mbele hadi Aprili 21 na 22 mwaka huu.
Ofisa Habari wa TFF Boniface Wambura alisema jana kwamba
Kamati ya Utendaji ya Shirikisho hilo iliyokutana Machi 10 mwaka huu jijini Dar
es Salaam chini ya uenyekiti wa Rais Leodegar Tenga uliamua kusogeza mbele
Mkutano Mkuu kutokana na mtiririko wa matukio ndani ya TFF katika kipindi
hicho.
Alisema katika mkutano huo mkuu kutakuwa na ajenda 25
mbalimbali katika Mkutano Mkuu huo wa kawaida wa TFF zikiwemo kufungua kikao,
kuthibitishwa kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu, kuthibitisha muhtasari wa Mkutano
Mkuu uliopita na yatokanayo na muhtasari
wa kikao kilichopita.
Pia kutakuwa na hotuba
ya Rais, kupokea taarifa za utekelezaji za wanachama na kupokea taarifa ya
utekelezaji ya Kamati ya Utendaji,
kupitisha taarifa ya ukaguzi wa hesabu za mwaka uliopita, kupitisha
taarifa ya wakaguzi wa hesabu na hatua zilizochukuliwa na kupitisha bajeti ya mwaka 2012.
“Ajenda nyingine ni
kupitisha mapendekezo ya marekebisho ya Katiba ya TFF, kujadili
mapendekezo yaliyowasilishwa na Wanachama au Kamati ya Utendaji, mengineo na
kufunga kikao,”Alisema Wambura.


.png)
0 comments:
Post a Comment