• HABARI MPYA

    Saturday, March 31, 2012

    MAFISANGO NAYE ABWAGA MANYANGA SIMBA

    MafisangoMAFISANGO

    KUFUATIA kusimamishwa na uongozi wa Simba, Patrick Mafisango, sasa anataka alipwe fedha zake ili arudi kwao Rwanda.
    Kiungo huyo Mnyarwanda mwenye asili ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, alisimamishwa kutokana na makosa ya utovu wa nidhamu.
    Inadaiwa aliripoti kambini Jumatano iliyopita akiwa amelewa chakari na alinaswa na Meneja, Nico Nyagawa. Kambi ya timu hiyo iko Bamba Beach, Kigamboni, jijini Dar es Salaam.
    Inasemekana badala ya kujieleza kwa uungwana, Mafisango alianza kumrushia matusi Nyagawa.
    Alipokuwa akielekea chumbani, alikutana na kocha Milovan Cirkovic, ambaye naye alimhoji.
    Imeelezwa kuwa Mafisango pia alimtukana na Mserbia huyo, ambaye aliutaarifu uongozi uliofikia uamuzi huo wa kumwondoa kambini.
    Akizungumza na Mwanaspoti, Mafisango alisema: "Nimechoka na majungu, kuna watu wachache wanataka kuniharibia jina langu.
    "Ninachotaka sasa, Simba inilipe haki zangu zilizobaki kabla ya mkataba wangu kuisha, nauli ya mtoto (Crespo), mke wangu na mimi, nirudi nyumbani nikafanye mambo mengine.
    "Nimevumilia sana, naambiwa ni mlevi na mambo kibao ambayo kwa kipindi kirefu navumilia. Majungu haya ndiyo nasikia hapa Tanzania, mbona nimecheza timu mbalimbali, Rwanda na Congo hakukuwa na matatizo?"
    Mafisango pia alitemwa na Azam kutokana na matatizo hayo ya utovu wa nidhamu.
    Hata hivyo, Milovan alitetea msimamo wa kumtimua Mafisango akisema hawezi kuvumilia mchezaji asiyekuwa na nidhamu.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAFISANGO NAYE ABWAGA MANYANGA SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top