• HABARI MPYA

    Tuesday, February 14, 2023

    RAIS SAMIAH AAHIDI DONGE NONO SIMBA NA YANGA


    RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, DK. Samiah Suluhu Hassan ameahidi kulipia Sh. Milioni 5 kila goli watakalofunga Simba na Yanga kwenye mechi zao za hatua ya makundi michuano ya klabu barani Afrika wikiendi hii.
    Simba watakuwa wenyeji wa Raja Casablanca Jumamosi na Yanga watawakaribisha TP Mazembe Jumapili, mechi zote zikipigwa Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Kikosi cha Simba kimerejea leo nchini tayari kuanza maandalizi ya mchezo wake wa pili wa Kundi C Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Raja Casablanca Jumamosi Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Ikumbukwe mechi za kwanza, Raja iliichapa Vipers ya Uganda 5-0 Jijini Casablanca na Simba ilifungwa 1-0 na Horoya Uwanja wa Jenerali Lansana Conte Jijini Conakry nchini Guinea. Vipers watakuwa wenyeji wa Horoya Jumamosi.
    Kwa upande wao, Yanga wamerejea leo nchini na moja kwa moja kuingia kambini kujiandaa na mchezo wa pili wa Kundi D Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya TP Mazembe ya DRC Jumapili Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Ikumbukwe mechi za kwanza Jumapili, Yanga ilichapwa 2-0 na wenyeji, US Monastirienne Uwanja wa Olimpiki Hammadi Agrebi Jijini Radès, Tunis nchini Tunisia na Mazembe iliichapa Real Bamako 3-1 Jijini Lubumbashi. Jumapili pia Real watakuwa wenyeji wa Monastir.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: RAIS SAMIAH AAHIDI DONGE NONO SIMBA NA YANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top