• HABARI MPYA

    Thursday, November 01, 2018

    SAMATTA AFUNGA MABAO MAWILI KRC GENK YATOKA NYUMA KWA 2-0 NA KUSHINDA 4-2 LIGI YA UBELGIJI

    Na Mwandishi Wetu, DEURNE
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta usiku wa jana amefunga mabao mawili katika ushindi wa 4-2 wa klabu yake, KRC Genk dhidi ya Royal Antwerp FC kwenye mchezo wa ugenini wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji, maarufu kama Jupiler Pro League.
    Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Bosuil mjini Deurne, Samatta alifunga mabao yake dakika za 76 na 90, baada ya kiungo wa kimataifa wa Ukraine, Ruslan Malinovskiy kutangulia kuifungia Genk mabao mawili dakika za 56 na 60 na yote kwa penalti.
    Mabao ya Malinovskiy yalikuwa ya kusawazisha baada ya wenyeji, Royal Antwerp FC kumaliza kipindi cha kwanza wanaongoza 2-0 kwa mabao ya mshambuliaji kutoka Jamhuri ya Kidemkrasia ya Kongo (DRC) Jonathan Bolingi Mpangi Merikani dakika ya 23 na kiungo Mnorway, Simen Juklerod dakika ya 45 na ushei.
    Mbwana Samatta akishangilia baada ya kuifungia KRC Genk mabao mawili katika ushindi wa 4-2 dhidi ya Royal Antwerp FC 
    Mbwana Samatta akishangilia na wenzake baada ya kuifungia KRC Genk mabao mawili jana
    Mbwana Samatta (kulia) akimtoka beki wa Royal Antwerp FC jana
    Mbwana Samatta akiondoka baada ya kufunga huku kipa wa Royal Antwerp FC, Vukovic akiwa hoi
    Mbwana Samatta (kulia) akiwa na wachezaji wenzake walioanza jana dhidi ya Royal Antwerp FC 

    Kwa Samatta jana amefikisha mechi 126 katika mashindano yote tangu amejiunga na Genk Januari mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na amefunga jumla ya mabao 50.
    Katika Ligi ya Ubelgiji amecheza mechi 98 na kufunga mabao 36, Kombe la Ubelgiji mechi nane mabao mawili na Europa League mechi 20 mabao 14.
    Kikosi cha Royal Antwerp FC kilikuwa; Bolat, Opare/Owusu dk82, Juklerod, Rodrigues/Baby dk86, Bolingi, Refaelov/Hairemans dk77, Arslanagic, Buta, Van Damme, Haroun na Mbokani.
    KRC Genk; Vukovic, Maehle, Aidoo, Dewaest, Urones, Heynen, Pozuelo/Berge dk72, Malinovskyi, Zhegrova/Seck dk82, Paintsil/Ndongala dk55 na Samatta.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA AFUNGA MABAO MAWILI KRC GENK YATOKA NYUMA KWA 2-0 NA KUSHINDA 4-2 LIGI YA UBELGIJI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top