• HABARI MPYA

    Tuesday, August 20, 2013

    WAKALI WAPYA WA SIMBA SC, KAZE NA TAMBWE WAIFUATA TIMU KAHAMA TAYARI KWA MCHEZO WA KWANZA WA LIGI KUU DHIDI YA RHINO

    Na Mahmoud Zubeiry, IMEWEKWA AGOSTI 20, 2013 SAA 8:20 MCHANA
    WACHEZAJI wawili wa kimataifa wa Burundi, beki Kaze Gilbert na mshambuliaji Tambwe Amisi wamewasili jana usiku Dar es Salaam kujiunga na klabu ya Simba SC na kesho watapanda ndege kwenda kuungana na timu kambini, Kahama wakipitia Mwanza.
    Simba SC imeweka kambi Kahama mkoani Shinyanga kujiandaa na mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Rhino Rangers Uwanja wa Ally Hassan Mwinyi mjini Tabora, Jumamosi.
    Wakali wawili; Kaze Gilbert kulia akipata chakula cha mchana na Tambwe Amisi, Mlimani City, Dar es Salaam leo. 

    Na wachezaji hao waliochelewa kwa sababu ambazo hazikuwekwa bayana, wataungana na kikosi cha Alhaj Abdallah Athumani Seif ‘King Kibaden’ tayari kuanza kazi Msimbazi.
    Wawili hao ndio pekee waliokuwa wanasubiriwa kukamilisha kikosi kizima cha Wekundu wa Msimbazi, tayari kwa mbio za ubingwa wa Ligi Kuu msimu huu.
    Wote wamesajiliwa kutoka Vital’O ya Burundi, mabingwa wapya wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame katika michuano iliyofanyika Sudan mwaka huu.
    Tambwe aliibuka mfungaji bora wa mashindano hayo ambayo timu za Tanzania, Simba SC na waliokuwa mabingwa watetezi, Yanga SC zilijitoa kwa kuhofia machafuko yaliyokuwa yakiendelea nchini humo. 
    Kaze aliibuka beki bora wa mashindano hayo, yaliyoshuhudia Vital’O ikitwaa taji lake la kwanza kabisa la michuano hiyo, licha ya kwamba ni timu kongwe kwenye mashindano hayo ya CECAFA.
    Wawili hao wanafikisha idadi ya wachezaji wanne wa kigeni wa Simba SC, kasoro mmoja kufika kikomo kwa mujibu wa kanuni za Ligi Kuu, baada ya Waganda, kipa Abbel Dhaira na beki Joseph Owino.
    Simba SC imepanga kukamilisha idadi ya wachezaji wa kigeni kwa kumsaini Moses Oloya anayecheza Vietnam kwa sasa ambaye pia anawaniwa na mahasimu wao, Yanga SC. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: WAKALI WAPYA WA SIMBA SC, KAZE NA TAMBWE WAIFUATA TIMU KAHAMA TAYARI KWA MCHEZO WA KWANZA WA LIGI KUU DHIDI YA RHINO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top