• HABARI MPYA

    Sunday, February 11, 2024

    YANGA SC YAICHAPA TANZANIA PRISONS 2-1 PATI LA MIAKA 89 LAFANA SOKOINE


    MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya wenyeji, Tanzania Prisons katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara leo uliokwenda sambamba na sherehe za miaka 89 ya vigogo hao wa kabumbu nchini Uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya.
    Kiungo Peodoh Pacôme Zouzoua  alianza kumsetia mshambuliaji mzawa, Clement Francis Mzize kuifungia Yanga bao la kwanza dakika ya nane, kabla ya yeye mwenyewe kufunga la pili dakika ya 45 akimalizia pasi ya Muivory Coast mwenzake, beki wa kulia Kouassi Attohoula Yao.
    Yanga ikapata pigo dakika ya 58 baada ya kipa wake Metacha Boniphace Mnata kutolewa kwa kadi nyekundu kwa kumchezea rafu mshambuliaji wa Tanzania Prisons nje kidogo ya boksi.
    Kipa Abdultwalib Hamidu Mshery akaingia baada ya kutolewa kiungo Farid Mussa Malik kabla ya mshambuliaji Jeremiah Juma Mgunda kufunga kwa mpira wa adhabu kwa urahisi dakika ya 64.
    Tanzania Prisons nao wakampoteza kiungo Zabona Khamis Mayombya aliyetolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 86 kufuatia kuonyeshwa kadi ya pili ya njano akidaiwa kujiangusha wakati anadhibitiwa na Nahodha wa Yanga, Bakari Nondo Mwamnyeto.
    Kwa ushindi huo, Yanga SC inafikisha pointi 40 katika mchezo wa 15 na kuendelea kuongoza Ligi, ikifuatiwa na Azam FC yenye pointi 32 za mechi 14 na Simba SC pointi 30 za mechi 14.
    Kwa upande wao Tanzania Prisons baada ya kupoteza mchezo wa leo inabaki na pointi zake 17 za mechi 26 sasa nafasi ya tisa
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YAICHAPA TANZANIA PRISONS 2-1 PATI LA MIAKA 89 LAFANA SOKOINE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top