• HABARI MPYA

    Monday, December 28, 2015

    SIMBA SC YATUPWA NJE MBIO ZA UBINGWA, KAGERA, MBEYA CITY ‘ZACHUNGULIA KABURI’

    RATIBA LIGI KUU YA VODACOM TZ BARA
    Desemba 30, 2015
    Azam FC vs Mtibwa Sugar
    Januari 1, 2015
    Ndanda FC vs Simba SC
    Januari 16, 2016
    JKT Ruvu vs Mgambo JKT
    Toto Africans vs Prisons
    Simba SC vs Mtibwa Sugar
    Stand United vs Kagera Sugar
    Mbeya City vs Mwadui FC
    Coastal Union vs Majimaji
    Azam FC vs African Sports
    Januari 17, 2016
    Yanga SC vs Ndanda FC
    Kikosi cha Simba SC kilichotoa sare ya 1-1 na Mwadui FC Jumamosi Uwanja wa Kambarage, Shinyanga

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SARE tatu mfululizo, rasmi zinatosha kuiondoa Simba SC katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na kwa mara nyingine inaziacha Azam na Yanga SC ziwanie taji.
    Simba SC ililazimishwa sare ya 1-1 na Mwadui FC Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga Jumamosi na hivyo kufikisha pointi 24 baada ya kucheza mechi 12.
    Simba SC sasa inashika nafasi ya nne katika msimamo wa Ligi Kuu, nyuma ya Mtibwa Sugar wenye pointi 27 za mechi 13 pia, wakati Azam FC yenye pointi 32 za mechi 12 ni ya pili na mabingwa watetezi, Yanga SC wanaongoza kwa pointi zao 33 za mechi 13.
    Kocha Muingereza, Dylan Kerr aliyetoa sare ya 2-2 na Azam FC, 1-1 na Toto na 1-1 Mwadui ndani ya wiki mbili, mwishoni mwa wiki atakuwa na mchezo wa kiporo dhidi ya Ndanda FC mjini Mtwara.
    Na Desemba 30, Azam FC nao watacheza kiporo chao dhidi ya Mtibwa Sugar na baada ya hapo kila timu itakuwa imecheza mechi 13 za Ligi Kuu, inayoshirikisha timu 16.
    Hali itakuwa mbaya kwa kocha Kerr iwapo Simba SC itacheza mechi ya nne bila kushinda Januari 1, 2016 na inawezekana kabisa uongozi wa klabu, chini ya Rais, Evans Aveva ukachukua maamuzi magumu.
    Wakati hali ikiwa mbaya kwa Simba SC, ushindani wa taji unazidi kunoga baina ya Azam FC na Yanga SC, baada ya timu zote kushinda mechi zao za mwishoni mwa wiki.
    Yanga SC ilianza kuifunga 3-0 Mbeya City Jumamosi na jana Azam FC wakaifunga Kagera Sugar 2-0. Yanga SC watakuwa mapumzikoni wiki hii, wakati Azam FC wakicheza na Mtibwa kumalizia kiporo chao ili mbio ziende vizuri.
    African Sports iliyorejea Ligi Kuu msimu huu inaburuza mkia ikiwa imeambulia pointi saba katika mechi 13, juu yake kuna Kagera Sugar yenye pointi tisa sawa na Coastal Union na Ndanda FC baada ya timu zote kucheza mechi 13.
    Hali si shwari pia kwa Majimaji yenye pointi 11 sawa na Mbeya City, JKT Ruvu pointi 12 na Mgambo JKT pointi 13 baada ya timu zote kucheza mechi 13.   
    Toto Africans yenye pointi 17, Prisons pointi 21, Stand United pointi 22 sawa na ndugu zao, Mwadui FC – hizo zipo sehemu salama kidogo, kwamba zinaweza kubaki Ligi Kuu.
      • Blogger Comments
      • Facebook Comments

      0 comments:

      Item Reviewed: SIMBA SC YATUPWA NJE MBIO ZA UBINGWA, KAGERA, MBEYA CITY ‘ZACHUNGULIA KABURI’ Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
      Scroll to Top