• HABARI MPYA

    Saturday, November 15, 2014

    UGANDA WAICHAPA 1-0 GHANA KAMPALA NA KUNUSA FAINALI ZA MATAIFA YA AFRIKA

    Na Ayesha Mugabi, KAMPALA
    BAO pekee la Savio Kabugo dakika ya tisa, limeipa Uganda ushindi wa 1-0 Uwanja wa Mandela, Namboole mjini Kampala, dhidi ya Ghana katika mchezo wa Kundi E kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika mwakani.
    Ushindi huo, unaifanya The Cranes inayofundishwa na Mserbia, Milutin Sredojevic ‘Micho’ itimize pointi saba baada ya kucheza mechi tano sawa na Black Stars, walio kileleni kwa pointi nane. 
    Mechi nyingine zilizopigwa leo, Afrika Kusini imeilaza 2-1 Sudan Uwanja wa Moses Mabhida, mechi ya Kundi A.
    Mfungaji wa bao pekee la Uganda leo, Savio Kabugo

    Mabao ya Bafana Bafana yamefungwa na Thulani Serero dakika ya 38 na Tokelo Rantie dakika ya 53, wakati bao pekee la Sudan limefungwa na Salah Ibrahim dakika ya 77.
    Bafana sasa inatimiza pointi 11 kileleni baada ya mechi tano, ikifuatiwa na Kongo yenye pointi saba za mechi nne sawa na Nigeria yenye pointi nne, wakati Sudan inabaki na pointi zake tatu licha ya kucheza mechi tano. 
    Malawi imepata ushindi wa 2-0 dhidi ya Mali Uwanja wa Kamuzu mjini Blantyre, mabao ya Robert Ng'ambi dakika ya 64 na Esau Kanyenda dakika ya 85.
    Malawi inatimiza pointi sita baada ya mechi tano na kubaki nafasi ya tatu, nyuma ya Mali pointi sita pia na Algeria inayoongoza kwa pointi zake 12 katika Kundi B.  
    Mechi za jana, Botswana ilitoka 0-0 na Tunisia Uwanja wa Taifa wa Gaborone, mchezo wa Kundi G, wakati Ivory Coast ilipata ushindi mzuri ugenini wa 5-1 dhidi ya Sierra Leone.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: UGANDA WAICHAPA 1-0 GHANA KAMPALA NA KUNUSA FAINALI ZA MATAIFA YA AFRIKA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top