• HABARI MPYA

    Wednesday, November 26, 2014

    EMERSON ATUA YANGA NA KUSEMA; “NIMEKUJA KUPAMBANA”

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    KIUNGO mkabaji Mbrazil, Emerson Oliveira Neves Roque amewasili mjini Dar es Salaam mchana wa leo tayari kufanya majaribio ya kujiunga na klabu ya Yanga SC.
    Baada ya kuwasili akiwa ameongozana na Wabrazil wenzake ambao tayari wanapiga kazi Jangwani, Kocha Marcio Maximo na kiungo mshambuliaji Andrey Coutinho, mchezaji huyo alisema; “Ninafurahi kuwa Tanzania, na niko tayari kupambana,”.
    Emerson mwenye umbo kubwa mithili ya mchezaji mpya wa Azam FC, Serge Wawa Pascal raia wa Ivory Coast, hakuzungumza sana, lakini Maximo alizungumza pia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, (JNIA) Dar es Salaam. 
    Emerson akiwa na Meneja wa Yanga SC, Hafidh Saleh kulia baada ya kuwasili JNIA leo

    “Nimefurahi kuja naye huyu mchezaji hapa, kwa sababu ninamjua ni mtu wa kazi, kinachofuata atazungumza na uongozi, kisha ataanza majaribio,”alisema Maximo.
    Kocha huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars amesema kwamba Yanga ni timu kubwa yenye wachezaji wengi wenye uwezo mkubwa, hivyo Emerson anatakiwa kupambana. 
    Emerson anakuja kuchukua nafasi ya mshambuliaji Genilson Santana Santos ‘Jaja’ aliyejiondoa Yanga kwa matatizo ya kifamilia.
    Emerson mwenye umri wa miaka 24 mzaliwa wa Rio de Janeiro, anakuja Yanga SC akitokea klabu ya 
    Bonsucesso ya mjini humo, ambayo imewahi kucheza Ligi ya Serie B mara mbili, ingawa kwa sasa inacheza ligi ya jimbo la Rio.
    Mchezaji huyo anatarajiwa kuanza majaribio kesho na akifuzu atafanyiwa vipimo vya afya, kabla ya kusajiliwa. Wazi mchezaji huyo ana nafasi ya kusajiliwa Yanga SC kwa kuwa analetwa na kocha Maximo, ambaye tayari amemsifia ni mtu wa kazi.
    Jaja alijiunga na Yanga SC msimu huu, lakini hakuwahi kuwavutia wapenzi wa klabu hiyo, ingawa atakumbukwa kwa mabao yake mawili aliyofunga wakati Yanga SC ikiifunga Azam FC 3-0 katika mechi ya Ngao ya Jamii Septemba 14, mwaka huu.
    Kwa ujumla, katika mechi 11 Jaja aliifungia mabao sita Yanga SC, moja katika mechi saba za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na matatu katika michezo ya kirafiki mbali na hayo mawili yaliyopeleka Ngao ya Jamii Jangwani.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: EMERSON ATUA YANGA NA KUSEMA; “NIMEKUJA KUPAMBANA” Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top