• HABARI MPYA

    Sunday, June 03, 2018

    UMTITI AWAKATAA MAN UTD, AONGEZA MKATABA BARCA HADI 2023

    BEKI Samuel Umtiti amesaini mkataba mpya wa miaka mitano kuendelea kuichezea Barcelona baada ya kukataa kujiunga na Manchester United.
    Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ufaransa mwenye umri wa miaka 24 alikuwa anaweza kuuzwa kwa Pauni Milioni 53 katika mkataba wake wa awali, ambayo ilimvutia kocha Jose Mourinho kutaka amchukue kuimarisha safu yake ya ulinzi.
    Lakini Umtiti atabaki Nou Camp baada ya kusaini mkataba wa hadi mwaka 2023 ambao utamfanya awe analipwa mshahara mara mbili ya aliokuwa analipwa.

    Beki wa Ufaransa, Samuel Umtiti ameongeza mkataba Barcelona hadi mwaka 2023 PICHA ZAIDI GONGA HAPA 

    Umtiti, aliyejiunga na Barcelona mwaka 2016 akitokea Lyon kwa dau la Pauni Milioni 20, alikuwa sehemu ya mafanikio ya kikosi hicho kutwaa mataji mawili ya nyumbani msimu uliomalizika.
    Alicheza mechi 40 kwenye mashindano yote, zikiwemo tisa za Ligi ya Mabingwa Ulaya ambako Barcelona ilitolewa na Roma kwenye Nusu Fainali.
    Umtiti pia alishinda taji la Kombe la Mfalme, maarufu kama Copa del Rey katika msimu wake wa kwanza na pia ameichezea jumla ya mechi 18 timu ya taifa ya Ufaransa.
    Ameitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Ufaransa kwa ajili ya Fainali za Kombe la Dunia nchini Urusi baadaye mwezi huu nchini Urusi ambako timu yake ni miongoni mwa zinazopewa nafasi ya kutwaa taji.
    Baada ya kushindwa kumuhamishia Umtiti Old Trafford, United sasa watajaribu kutaka kuimarisha kikosi chao kwa kumsajili Toby Alderweireld kutoka Tottenham ambaye thamani yake ni Pauni Milioni 55.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: UMTITI AWAKATAA MAN UTD, AONGEZA MKATABA BARCA HADI 2023 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top