• HABARI MPYA

    Friday, March 08, 2019

    AZAM FC YAPATA USHINDI WA KISHINDO LIGI KUU, YAITANDIKA JKT TANZANIA 6-1

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Azam FC imepata ushindi wa kishindo wa mabao 6-1 dhidi ya JKT Tanzania katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara usiku wa leo Uwanja wa Azam Complex, Chamazi mjini Dar es Salaam.
    Mshambuliaji Mzimbabwe, Donald Dombo Ngoma ametokea benchi kipindi cha pili na kuifungia Azam FC mabao mawili dakika ya 60 na 78.
    Mabao mengine ya Azam FC yamefungwa na Aggrey Morris dakika ya 16, Mudathir Yahya dakika ya 26, Obrey Chirwa dakika ya 74 na Daniel Lyanga dakika ya 88, wakati bao pekee la JKT limefungwa na Hassan Matalema dakika ya 81.

    Kwa ushindi huo, Azam FC inafikisha pointi 56 katika mechi ya 27 ikiendelea kushika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu inayoshirikisha timu 20.  
    Yanga SC wanaendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi zao 64 baada ya kucheza mechi 26 na mabingwa watetezi, Simba SC wanaendelea kukamata nafasi ya tatu kwa pointi zao 51 za mechi 20.
    Ligi Kuu itaendelea kesho kwa mechi tatu zaidi, Mtibwa Sugar wakiikaribisha Stand United Uwanja wa Manungu, Turiani mkoani Morogoro, Kagera Sugar wakiwa wenyeji wa Coastal Union Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba na Lipuli FC wakiwa wenyeji wa Mbao FC Uwanja wa Samora mjini Iringa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC YAPATA USHINDI WA KISHINDO LIGI KUU, YAITANDIKA JKT TANZANIA 6-1 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top