• HABARI MPYA

    Thursday, March 21, 2019

    MAYANGA ACHUKUA NAFASI YA ALLY BUSHIRI MBAO FC AIPIGANIE KUBAKI LIGI KUU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    ALIYEWAHI kuwa kocha wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Salum Mayanga ameingia mkataba wa kufundisha klabu ya Mbao FC ya Mwanza hadi mwishoni mwa msimu.
    Mayanga, mchezaji na kocha wa zamani wa klabu ya Mtibwa Sugar ya Morogoro, anakwenda kuchukua nafasi ya Ally Bushiri ‘Bush’ aliyeondolewa kutokana na matokeo mabaya.
    Bushiri, Kocha Msaidizi wa zamani wa Taifa Stars ameondolewa Mbao FC aliyojiunga nayo Januari mwaka huu baada ya kuondoka kwa Amri Said ‘Stam’ kutokana na timu hiyo kufanya vibaya.

    Salum Mayanga amechukua nafasi ya klabu ya Ally Bushiri klabu ya Mbao FC ya Mwanza 

    Pamoja na kutolewa katika michuano ya Azam Sports Federation Cup (ASFC), mwenendo wa Mbao FC katika Ligi Kuu ya Tanzania Bara si mzuri chini ya Bushiri.
    Bushiri anaiacha Mbao FC katika nafasi ya 14 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya timu 20, ikiwa na pointi 36 baada ya kucheza mechi 20, pointi sita tu zaidi ya Biashara United ya Mara inayoshika nafasi ya 19.   
    Baada ya kuondolewa timu ya taifa Machi mwaka jana, Mayanga alirejea Mtibwa Sugar kama Mshauri wa Ufundi wa Kocha Mkuu, Zubery Katwila.
    Msimu huu, timu mbili zitashuka moja moja kwa moja kutoka Ligi Kuu na washindi wa kwanza wa makundi mawili ya Daraja la Kwanza watapanda moja kwa moja.
    Timu zitakazoshika nafasi ya pili na ya tatu Kundi A na B Daraja la Kwanza zitamenyana na washindi wawili watakwenda kumenyana na timu zitakazoshika nafasi ya 17 na 18 Ligi Kuu na washindi wa mechi hizo watacheza Ligi Kuu msimu ujao kukamilisha idadi ya timu 20 kama kawaida.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAYANGA ACHUKUA NAFASI YA ALLY BUSHIRI MBAO FC AIPIGANIE KUBAKI LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top