• HABARI MPYA

    Friday, February 04, 2022

    NI MISRI YA SALAH NA SENEGAL YA MANE FAINALI AFCON


    TIMU ya taifa ya Misri imefanikiwa kwenda Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya ushindi wa penalti 3-1 kufuatia sare ya bila kufungana na wenyeji, Cameroon ndani ya dakika ya 120 usiku wa Alhamisi Uwanja wa Paul Biya Jijini Yaoundé.
    Kipa wa klabu ya Zamalek, Mohamed Abou Gaba ‘Gabaski’ ndiye aliyeibuka shujaa wa Mafarao kwa kucheza penalti mbili za nyota wa Simba Wasiofungika, Harold Moukoudi na James Lea Siliki, wakati mkwaju wa zamani wa Tottenham Hotspur, Clinton N'Jie uliota mbaya.
    Waliofunga penalti za Misri ni
    Ahmed Mostafa Mohamed ‘Zizo’,  Mohamed Abdelmonem na  Mohanad Lasheen na sasa Mafarao watakutana na Senegal katika Fainali tamu ya AFCON 2021 Jumapili hapo hapo Paul Biya .
    Kocha wa Mreno wa Misri, Carlos Queiroz alitolewa kwa kadi nyekundu na refa Mgambia, Bakary Papa Gassama baada ya kupingana na maamuzi kipindi cha pili.
    Utakuwa usiku mzuri wa kuwashudia washambuliaji wawili nyota wa Liverpool, Mohamed Salah wa Misri na Sadio Mane wa Senegal wakiyapigania mataifa yao baina yao uwanjani.
    Cameroon watajaribu kupoza machungu kwa kumenyana na Burkina Faso katika mechi y kuwania nafasi ya tatu, ambayo itachezwa Jumamosi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NI MISRI YA SALAH NA SENEGAL YA MANE FAINALI AFCON Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top